Saturday 10 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Kikosi cha Wachezaji 22 cha Man United kwenda USA
Sir Alex Ferguson ataongoza Kikosi cha Wachezaji 22 Siku ya Jumatatu Julai 12 kwenda kwenye ziara ya Marekani, Canada na Mexico itakayomalizika Julai 30.
Kikosi hichi ni mchanganyiko wa Wakongwe na Chipukizi ambamo Wakongwe ni kina Edwin van der Sar, Ryan Giggs na Paul Scholes na Vijana ni kina Corry Evans, Ben Amos na Tom Cleverley.
Wachezaji waliokuwa kwenye Kombe la Dunia huko Afrika Kusini, Wayne Rooney, Michael Carrick, Patrice Evra na Nemanja Vidic, hawatakuwemo kwani wapo likizo.
Mchezaji mpya ambae aliiwakilisha Mexico kwenye Kombe la Dunia, Javier Hernandez, atajiunga na wenzake Julai 27 huko Houston, USA.
Nahodha Gary Neville hatakuwemo kwenye Kikosi hicho kwa vile ana tatizo la musuli za mguu.
Man United watatua kwanza huko Chicago na kupiga kambi ya mazoezi na mechi yao ya kwanza itakuwa dhidi ya Celtic ya Scotland huko Toronto, Canada hapo Julai 16.
Halafu watasafiri hadi Philadelphia, USA kucheza na Philadelphia United hapo Julai 21 na Julai 25 watakuwa Kanasas City kucheza na Kansas City Wizards.
Kisha wataenda Houston kucheza na Kombaini ya Mastaa wa MLS, Ligi ya huko Marekani.
Ziara ya Man United itamalizikia huko Mexico Julai 30 watakapocheza na Timu ya zamani ya Javier Hernandez, Chivas, Mjini Guadalajara.
Kikosi kamili: Edwin van der Sar, Tomasz Kuszczak, Paul Scholes, Ryan Giggs, Dimitar Berbatov, John O'Shea, Wes Brown, Rafael, Jonny Evans, Darren Fletcher, Darron Gibson, Chris Smalling, Nani, Fabio, Federico Macheda, Danny Welbeck, Javier Hernandez (atajiunga Julai 27 huko Houston), Mame Biram Diouf, Tom Cleverley, Ritchie De Laet, Corry Evans, Ben Amos, Gabriel Obertan.
CHEKI: www.sokainbongo.com

NI FAINALI!!!
Holland v Spain
Uwanja: Soccer City, Soweto, Johannesburg
Jumapili, Julai 11 Saa 3.30 usiku [bongo]
Kesho, pazia la kufunga Mashindano ya Kombe la Dunia 2010 iliyofanyika huko Afrika Kusini kuanzia Juni 11, ikiwa ni mara ya kwanza kwa Kombe la Dunia kuchezwa Afrika, litafungwa.
Kwa ujumla, Mashindano haya yameleta msisimko mkubwa hasa kwa vile Timu zile Vigogo zote, kama Italy, Brazil, Argentina na Ujerumani,  zilibwagwa nje nyingine zilitolewa mapema mno.
Holland:
-Meneja: Bert van Marwijk
-Listi ya FIFA ya Ubora: nafasi ya 4
-Majeruhi: De Zeeuw
-Aliefungiwa: Hamna
Spain:
-Meneja: Vicente del Bosque
-Listi ya FIFA ya Ubora: nafasi ya 2
-Majeruhi: Albiol
-Aliefungiwa: Hamna
DONDOO ZA MECHI:
-Hii ni Fainali ya kwanza ya Kombe la Dunia ambayo haina moja ya Nchi za Brazil, Argentina, Italy au Germany.
-Ikiwa Spain watashinda, itakuwa Nchi ya kwanza kutwaa Kombe la Dunia baada ya kufungwa mechi yao ya kwanza kwenye mechi za Fainali. Juni 16, Spain walifungwa na Uswisi bao 1-0.
-Ikiwa Holland watashinda, watakuwa ni Nchi ya Pili [Brazil ya kwanza Mwaka 1970] kwa kushinda mechi zao zote za Kombe la Dunia kuanzia mechi za Mchujo.
-Spain wamecheza pasi 3,387 katika Fainali hizi ambazo ni nyingi kupita Timu yeyote.
-Wesley Sneijder amefunga bao 7 katika mechi zake za Kimataifa 8 zilizopita.
Timu: Wachezaji wanaotegemewa kuanza
Holland: Stelenburg, Heitinga, Mathijsen, Van der Wiel, Van Bronkhorst, Van Bommel, Sneijder, De Jong, Robben, Kuyt, Van Persie
Spain: Casillas, Pique, Puyol, Ramos, Capdevila, Busquets, Xavi, Alonso, Iniesta, Pedro, Villa
Refa: Howard Webb [England]

Friday 9 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

MECHI YA MSHINDI WA 3:
Germany v Uruguay
Jumamosi Julai 10 Saa 3.30 usiku [bongo]
Hali za Kila Timu:
Germany huenda wakamkosa Straika Miroslav Klose mwenye maumivu ya mgongo na hivyo, akiwa amefunga jumla ya mabao 14 kwenye Fainali za Kombe la Dunia zote alizocheza, huenda akaikosa nafasi ya kuifikia rekodi ya Ronaldo de Lima ya kufunga jumla ya mabao 15 kwenye Fainali za Kombe la Dunia.
Thomas Muller amemaliza kifungo chake cha mechi moja na bila shaka ataonekana dimbani.
Uruguay watamkaribisha tena Luis Suarez aliefungiwa mechi moja kwa kushika mpira kwa makusudi na kuwakosesha Ghana ushindi.
Pia Beki wao Jorge Fucile atarudi tena baada ya kumaliza kifungo chake.
Tathmini:
Hii ni mechi ambayo kila Timu haitaki kuicheza kwa vile kila Timu inataka iingie Fainali na kutwaa Kombe la Dunia.
Lakini safari hii Mabingwa mara 3 wa Kombe la Dunia, Germany, wataivaa Uruguay ambao ni Mabingwa mara mbili.
Hii ni mechi ambayo kila Kocha huwa na wakati mgumu kuwapa motisha Wachezaji wao baada ya kuvunjika moyo kwa kutoingia Fainali ya Kombe la Dunia.
Historia kati yao:
Hii ni mechi ya 10 kati yao na Uruguay ilishinda mechi ya kwanza kwa bao 4-1 Mwaka 1928 lakini hawajashinda tena kati mechi 8 zilizofuata.
Germany wameshinda mechi 6, suluhu 2 na wamefungwa moja.
Waamuzi:
Refa:Benito Archundia (Mexico)
Wasaidizi: Hector Vergara (Canada) & Marvin Torrentera (Mexico)
CHEKI: www.sokainbongo.com

Brazil yaanua Nembo ya Kombe la Dunia 2014
Brazil, ambao ndio watakuwa Wenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia Mwaka 2014, leo wameanua rasmi Nembo itayotumika kwenye Mashindano hayo.
Nembo hiyo inayoitwa ‘Msukumo’ [Inspiration] ina mchoro wa Mikono mitatu iliyoshikamana yanye umbo la Kombe la Dunia na una rangi za Kijani na Njano kama Bendera ya Brazil.
Uzinduzi wa Nembo hiyo umefanywa na Rais wa Brazil, Luiz Inacio Lula da Silva huko Johannesburg na kuhudhuriwa pia na Wachezaji wa zamani wa Brazil Carlos Alberto, Cafu na Romario pamoja na Kocha wa zamani wa Brazil, Carlos Alberto Parreira, ambae aliifundisha Bafana Bafana kwenye Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka huu huko Afrika Kusini.
Rais Lula, katika uzinduzi huo, alisema wana mzigo mkubwa kuyafanya Mashindano ya Mwaka 2014 yawe ya mafanikio kama hayo ya Afrika Kusini.
Lula alitamka: “Mafanikio ya Ndugu zetu wa Afrika ni changamoto kubwa kwa Brazil. Tutajifunza kutoka kwao.”
Nae Rais wa FIFA, Sepp Blatter, amesema Soka huko Brazil ni kama dini na ameisifia kwa kuipa umuhimu kuliko Nchi yeyote.
Brazil ni Mabingwa wa Dunia mara 5 na walikuwa Wenyeji wa Kombe la Dunia Mwaka 1950.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Pweza Paulo atabiri Spain Bingwa Duniani, Germany Mshindi wa 3!!!
Yule Pweza Paulo, aliejijengea umaarufu Duniani kwa kutabiri mechi za Kombe la Dunia zinazochezwa huko Afrika Kusini, leo akiwa laivu kwenye TV alitabiri Spain ndie atashinda Jumapili dhidi ya Holland na kutwaa Kombe la Dunia.
Pweza Paulo hutoa utabiri wake kwa kutumbukiziwa kwenye tangi lake la maji anakoishi glasi mbili zenye chakula ambapo kila glasi inakuwa na bendera ya Timu moja.
Leo Paulo alifuata glasi yenye bendera ya Spain akiashiria Spain ndio Mshindi.
Kwenye mechi kati ya Germany na Uruguay itakayochezwa Jumamosi kutafuta Mshindi wa Tatu, Pweza Paulo aliifuata glasi ya Germany.
Listi ya wanaowania Mpira wa Dhahabu Kombe la Dunia yatolewa
FIFA imetoa Listi ya Wachezaji 10 watakaogombea Tuzo ya Mpira wa Dhahabu wa Kombe la Dunia 2010 ambayoi hutunukiwa Mchezaji Bora wa Mashindano hayo.
Listi hiyo ya Wachezaji hao 10 ni:
-David Villa [Spain]
-Xavi [Spain]
-Andres Iniesta [Spain]
-Wesley Sneijder [Holland]
-Arjen Robben [Holland]
-Bastian Schweinsteiger [Germany]
-Mesut Ozil [Germany]
-Lionel Messi [Argentina]
-Diego Forlan [Uruguay]
-Asamoah Gyan [Ghana]
Listi nyingine iliyotolewa na FIFA inahusu Mchezaji Bora Kijana na wamo:
-Thomas Mueller [Germany]
-Andrew Ayew [Ghana]
-Giovani dos Santos [Mexico]
Washindi wa Tuzo hizo watatangzwa Jumapili mara baada ya Fainali ya Kombe la Dunia itakayochezwa kati ya Holland na Spain Uwanja wa Soccer Cuty, Soweto, Johannesburg.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Tusimtegemee Rooney!!
Darren Fletcher anaamini ikiwa watataka kutwaa tena Ubingwa wa Ligi Kuu England Manchester United itabidi waondoe lile tegemezi lao kwa Wayne Rooney pekee kuwafungia magoli.
Msimu uliokwisha Rooney alifunga jumla ya Mabao 43 katika Mashindano yote lakini Chelsea ndio wakaibuka Mabingwa na Man United wakamaliza nafasi ya pili.
Fletcher ametamka: “Kama Timu itabidi tuongeze bidii na Wachezaji waongeze ubora. Msimu uliokwisha tuliwaona Nani na Valencia wakiongeza ubora wao”
Pia aliisema Timu ya Msimu uliopita ilikuwa kwenye kipindi cha mpito na hivyo Msimu huu watatulia zaidi.
Pweza Paulo: Kutoa utabiri leo mechi ya kesho Germany v Uruguay!
Huko Oberhausen, Ujerumani, ndani ya Tangi lake la maji anakoishi, Pweza aitwae Paulo, ambae amejizolea sifa kubwa ya kuwa Mtabiri wa Soka, anangojewa kwa hamu kutoa utabiri wa Mechi ya kutafuta Mshindi wa Tatu wa Kombe la Dunia, kati ya Germany na Uruguay, itakayochezwa huko Afrika Kusini Siku ya Jumamosi.
Pweza Paulo alitabiri Spain itashinda Mechi kati ya Spain na Germany ya Nusu Fainali na kweli Spain ikashinda na kuwavunja moyo maelfu ya Wajerumani ambao baadhi walikasirishwa na kutishia kumkaanga na kumla.
Baadhi ya Magazeti huko Ujerumani yalibeba bango: ‘MHAINI!’
Awali Pweza huyo alitabiri sawa sawa kabisa Mechi zote za Germany za Kombe la Dunia huko Afrika Kusini ambazo Germany ilizifunga Australia, Ghana, England na Argentina, na pia alitabiri kipigo cha Germany toka kwa Serbia.
Sasa Paulo amepata umaarufu mkubwa Duniani na kuonyeshwa kwenye TV kubwa kama CNN na BBC na pia kutoka katika Magazeti kila kona ya Dunia.
Ulinzi umeimarishwa kwa Pweza Paulo na inadaiwa Serikali ya Germany inafikiria kumpa hadhi ya Kiumbe alie hatarini ili apate hifadhi bora.
Kwa sasa Dunia nzima inagonja utabiri wa Mechi mbili za Kombe la Dunia na hasa ile Fainali ya Jumapili kati ya Holland v Spain.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Kuyt: ‘Spain haitutishi!’
Dirk Kuyt ameiponda Germany kwa kucheza na woga walipokutana na Spain kwenye Nusu Fainali ya Kombe la Dunia huko Afrika Kusini na kutolewa kwa bao 1-0 na amedai kuwa Holland Jumapili kwenye Fainali wataingia kupambana na Spain wakiwa na nia ya kushambulia tu.
Holland wataingia mechi hiyo ya Fainali wakiwa hawajafungwa katika mechi zao 25 za mwisho huku wakiwa wameshinda mfululizo mechi 14 za Michuano ya Kombe la Dunia kuanzia hatua ya mchujo.
Kuyt amesema: “Hatuogopi hata chembe! Uliona Germany walivyowaogopa na nini kimewakuta. Sie tutashambulia na kasoro zao zitajitokeza. Hatuna Wachezaji waoga!”
Hii ni mara ya 3 kwa Holland kutinga Fainali za Kombe la Dunia lakini mara mbili walifungwa na kuukosa Ubingwa wa Dunia.
Nae Kocha wa Holland, Bert van Marwijk, amekiri kupata ushauri kutoka kwa Mastaa wa Uholanzi wa zamani kina Johan Cruyff na Ruud Gullit muda wote ambao wako Afrika Kusini.
Belhadj ahama Pompey kwenda Qatar
Beki wa Portsmouth kutoka Algeria, Nadir Belhadj, amejiunga na Klabu ya Qatar Al Sadd bila ya kutajwa dau na pia aina ya Mkataba.
Uhamisho huo umethibitishwa na Klabu hiyo ya Qatar ambayo imekiri walikuwa wakimwinda Belhadj kwa muda mrefu.
Belhadj, Miaka 28, alikuwa na Kikosi cha Algeria kilichotolewa kwenye Kombe la Dunia huko Afrika Kusini, na alijiunga na Portsmouth Mwaka 2009 toka Klabu ya Ufaransa Lens.

Thursday 8 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Hargreaves mashakani tena!
Owen Hargreaves ataukosa mwanzo wa Msimu mpya wa Ligi Kuu England utakaoanza Agosti 14 kwa sababu ya kuendelea kusumbuliwa na matatizo yake ya magoti na anategemewa kurudi kwa Daktari speshelisti aliemfanyia opersheni huko Marekani kwa uchunguzi zaidi.
Habari hizo za matatizo ya Hargreaves zilithibitishwa na Meneja wake wa Manchester United, Sir Alex Ferguson.
Kiungo huyo alikuwa nje ya uwanja kwa Miezi 18 baada ya kupasuliwa magoti yote mawili na Msimu uliokwisha alirudi uwanjani na kuichezea Man United mechi moja tu.
Jumatatu ijayo, Man United inasafiri hadi Marekani ili kuanza ziara yao ya mazoezi na mechi za kirafiki na pia watazuru Canada na Mexico.
Ferguson vilevile alitoboa kuwa Michael Owen amepona na yupo mazoezini.
Kuhusu Anderson alieumia vibaya goti, Ferguson amesema anaendelea vizuri na huenda akarudi Uwanjani Mwezi Septemba.
Jovanovic atua Anfield
Fowadi kutoka Serbia, Milan Jovanovic, ambae alifunga bao moja na la ushindi Serbia ilipoifunga Germany kwenye mechi ya Kombe la Dunia huko Afrika Kusini, amesaini Mktaba wa Miaka mitatu na Liverpool.
Jovanovic, Miaka 29, ni Mchezaji Huru baada ya Mkataba wake na Klabu ya Ubelgiji Standard Liege kumalizika mwishoni mwa Msimu uliopita.
Inasemekana, Rafael Benitez ndie alietaka Jovanovic aende Liverpool kabla yeye kujua atahamia Inter Milan na hilo liliibua hisia huenda Jovanovic akaenda Inter badala ya Liverpool ili kuungana na Benitez.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Webb wa England kuchezesha Fainali Kombe la Dunia
Refa wa England, Howard Webb, ameteuliwa kuchezesha Fainali ya Kombe la Dunia kati ya Holland na Spain Siku ya Jumapili Julai 11 huko Soccer City, Soweto, Johannesburg.
Mara ya mwisho kwa Refa wa Kiingereza kuchezesha Fainali ya Kombe la Dunia ilikuwa Mwaka 1974 Jack Taylor alipochezesha mechi kati ya Germany v Holland ambayo Germany walitwaa Ubingwa wa Dunia kwa kushinda 2-1.
Refa Howard Webb atasaidiwa na wenzake toka England, Michael Mullarkey na Darren Cann.
Mpaka sasa huko Afrika Kusini, Webb na Timu yake wamechezesha Mechi 3, Spain walipofungwa 1-0 na Uswisi, Slovakia walipoibwaga Italy 3-2 na Brazil kuifunga Chile 3-0.
Katika mechi hizo tatu, Webb hakutoa Kadi Nyekundu wala penalti.
Webb na Wasaidizi wake ndio waliochezesha Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI Mwezi Mei Inter Milan ilipoifunga Bayern Munich 2-0 huko Santiago Bernabeau na kutwaa Ubingwa wa Ulaya.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Pweza Mtabiri kuimarishiwa ulinzi!!
Yule Pweza, aitwae Paul, ambae anafugwa kwenye Zuu huko Ujerumani na ambae amekuwa akitabiri mechi za Fainali za Kombe la Dunia na kupatia matokeo ambapo juzi alitabiri kuwa Spain itaishinda Germany katika mechi ya Nusu Fainali na kweli Spain ikaifunga Germany 1-0, atawekewa ulinzi mkali baada ya kuzuka hofu kuna Watu wanamuwinda wamle ikiwa ni hasira ya Germany kufungwa.
Msimamizi wa Pweza huyo, Oliver Walenciak, amesema: “Wapo Watu wanataka kumla Pweza wetu! Sisi tupo kumlinda!”
Awali Mashabiki wa Argentina walimlaumu Pweza huyo kwa wao kupigwa 4-0 na Germany mechi ambayo pia alitabiri sawa sawa na wakatishia kumla.
Wenger kutoa tamko kuhusu Kipa Arsenal
Arsene Wenger amesema atatoa msimamo wake kuhusu nani atakuwa Kipa Nambari Wani wa Arsenal baada ya kukiri Kipa wa sasa Manuel Almunia huingiwa na mchecheto kwenye mechi kubwa.
Msaidizi wa Almunia ni Lukasz Fabianski lakini nae ameshindwa kumpiku Almunia kwani alipopata nafasi za kucheza amekuwa akifanya makosa makubwa yakiwemo makosa mawili kwenye mechi ya UEFA CHAMPIONS LIGI dhidi ya FC Porto Msimu uliokwisha.
Kumekuwa na tetesi Kipa wa Fulham Mark Schwarzer huenda akatua Ze Gunners.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Arsenal wapata Difenda
Arsenal wamemnyakua Beki Laurent Koscielny kutoka Klabu ya Lorient ya Ufaransa kwa dau ambalo halikutajwa.
Beki huyo Mfaransa amesifiwa na Meneja wa Arsenal Arsene Wenger kuwa ni Mpiganaji mzuri na ataziba vizuri pengo liloachwa na William Gallas na Mikel Silvestre ambao mikataba imekwisha na pia Senderos aliehamia Fulham.
Huyu ni Mchezaji wa pili kuchukuliwa na Arsenal baada ya Straika Marouane Chamakh kujiunga kutoka Bordeaux.
Moratti akiri Man United inamtaka Sneijder
Rais wa Inter Mila Massimo Moratti amekiri kuwa ni kweli Manchester United ina nia ya kumchukua Kiungo toka Uholanzi Wesley Sneijder.
Mbali ya kukiri hivyo, Moratti amedai Sneijder, Miaka 26, atabaki Inter Milan ambayo Msimu uliokwisha chini ya Kocha Jose Mourinho alitoa mchango mkubwa kwa Timu hiyo kubeba Trebo, yaani Ubingwa wa Serie A, Coppa Italia na UEFA CHAMPIONS LIGI.
FAINALI NI HOLLAND v SPAIN
Spain 1 Germany 0
Bao la kichwa la Carles Puyol la dakika ya 73 kufuatia kona limewafikisha Spain Fainali ya Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza katika historia yao na watakutana na Holland Jumapili huko Soccer City, Soweto, Johannesburg na Siku hiyo atapatikana Bingwa mpya wa Dunia kwa vile Spain na Holland hawajawahi kuchukua Kombe la Dunia hata mara moja.
Spain walitawala kwa kipindi kirefu mechi hii lakini walishindwa kabisa kuipenya ngome ya Germany huku Germany wakionekana ni hatari kwa mashambulizi ya kushtukiza.
Germany watakutana na Uruguay Jumamosi kupata Mshindi wa Tatu.
Timu:
Spain: Casillas, Sergio Ramos, Pique, Puyol, Capdevila, Busquets, Alonso, Iniesta, Xavi, Pedro, Villa.
Akiba: Valdes, Albiol, Marchena, Torres, Fabregas, Mata, Arbeloa, Llorente, Javi Martinez, Silva, Jesus Navas, Reina.
Germany: Neuer, Lahm, Friedrich, Mertesacker, Boateng, Khedira, Schweinsteiger, Trochowski, Ozil, Podolski, Klose.
Akiba: Wiese, Jansen, Aogo, Tasci, Kiessling, Badstuber, Kroos, Cacau, Marin, Gomez, Butt.

Wednesday 7 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Barca wakopa kulipa Wachezaji Mishahara!!
Rais mpya wa FC Barcelona, Sandro Rosell, amekiri walishindwa kuwalipa Wachezaji wao Mishahara ya Juni na imebidi wachukue mkopo Benki ili kuwalipa.
Sandro, alierithi wadhifa huo kutoka kwa Joan Laporta, amesema wamekopa Pauni milioni 125 ili kuhakikisha Wachezaji wanalipwa.
Amesema: “Tumeikuta Klabu ina madeni na haina mtiririko wa fedha. Imebidi tuchukue mkopo”
Hata hivyo, Sandro amedai Barca bado wana uwezo wa kumnunua Cesc Fabregas toka Arsenal kwa vile wanaingiza pesa na pia wamewauza Dmitro Chygrynskiy kwa Shakhtar Donetsk kwa Pauni milioni 12.5 na Yaya Toure kwa Manchester City kwa Pauni Milioni 20.
Pia Sandro amedai wanacho kitita cha zaidi ya Pauni Milioni 50 kununua Wachezaji wengine ikiwa Kocha Pep Guardiola atahitaji hilo.
Barcelona ndio Mabingwa wa Spain.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Ratiba ya Mechi za Ufunguzi Ligi Kuu England yapanguliwa!
Ili kukidhi mahitaji ya Stesheni za TV kurusha moja kwa moja matangazo ya mechi za Ligi Kuu, baadhi ya mechi za ufunguzi wa Msimu mpya wa 2010/11 zimebadilishwa Siku na saa.
Mechi ya kwanza kabisa ya Ligi Kuu itakuwa ni Jumamosi Agosti 14, saa 8 dakika 45 mchana kati ya Tottenham na Manchester City.
Mechi nyingine 6 Siku hiyo zitaanza saa 11 jioni na ya mwisho itakuwa saa 1 na nusu usiku wakati Mabingwa Chelsea watakapoanza kampeni ya kutetea Ubingwa wao kwa kuikaribisha Stamford Bridge Timu iliyopanda Daraja, West Bromwich Albion.
Jumapili, Agosti 15 kutakuwa na mechi moja tu nayo ni BIGI MECHI huko Anfield kati ya Liverpool na Arsenal itakayoanza saa 12 jioni na hii itakuwa ni mechi ya kwanza kwa Meneja mpya wa Liverpool Roy Hodgson alietokea Fulham.
Manchester United wataanza vita yao ya kulirudisha Taji Old Trafford kwa mechi hapo Old Trafford dhidi ya Timu iliyopanda Daraja Newcastle Siku ya Jumatatu Agosti 16 saa 4 usiku.
RATIBA KAMILI MECHI ZA UFUNGUZI:
[saa za bongo]
Jumamosi, 14 Agosti 2010
Tottenham v Man City, [saa 8.45 mchana]
[saa 11 jioni]
Aston Villa v West Ham,
Blackburn v Everton,
Blackpool v Wigan,
Bolton v Fulham,
Sunderland v Birmingham,
Wolverhampton v Stoke,
Chelsea v West Brom, [saa 1 na nusu usiku]
Jumapili, 15 Agosti 2010
Liverpool v Arsenal, [saa 12 jioni]
Jumatatu, 16 Agosti 2010
Man Utd v Newcastle, [saa 4 usiku]
CHEKI: www.sokainbongo.com

Pweza Mtabiri aitia kiwewe Germany!!!
Ni Pweza anaeitwa Paul na anafugwa kwenye Zuu, hifadhi ya Wanyama na Viumbe wa Majini huko Berlin , Ujerumani na amepata umaarufu mkubwa kwa kutabiri matokeo ya mechi za Soka.
Lakini juzi, huku akirushwa laivu na TV za Ujerumani, aliwastua Watu pale alipotabiri Spain ndio itashinda kwenye Mechi ya Nusu Fainali ya Kombe la Dunia dhidi ya Germany.
Kawaida, Pweza huyo hutoa utabiri wake kwa kutumbukiziwa kwenye Bwawa lake glasi mbili za chakula chake na kila moja ina Bendera ya Timu zinazocheza na atakayoifuata ili kuchukua chakula ndie Mshindi.
Paul alitoa utabiri wake baada ya kutumbukiziwa kwenye sanduku lake la maji anakoishi glasi mbili zenye chakula moja ikiwa na Bendera ya Germany na nyingine Bendera ya Spain lakini Pweza huyo akafuata chakula kilichomo kwenye glasi ya Spain na hivyo huashiria ushindi kwa Spain.
Katika Fainali za Kombe la Dunia huko Afrika Kusini, Pweza huyo ameshatoa utabiri uliokuja kuwa kweli mara 5 zikiwemo mechi za ushindi wa Ujerumani dhidi ya Australia, Ghana, England na Argentina na kipigo cha Ujerumani mikononi mwa Serbia.
Lakini Wajerumani wanafarijika kuwa mara pekee Paul alipotoa utabiri ambao haukutokea kuwa kweli ni wakati ule wa Fainali ya EURO 2008 ambapo alitabiri Germany itaifunga Spain na kuwa Bingwa wa Ulaya lakini ikaja Spain kuifunga Germany 1-0.
Safari hii, katika mechi ya Germany v Spain, ameitabiria Spain ushindi!! Je itakuwa kama 2008?
CHEKI: www.sokainbongo.com

NUSU FAINALI YA PILI:
Leo tena: German v Spain
Timu na Wachezaji:
Germany watamkosa tu Thomas Mueller ambae amefungiwa mechi moja baada ya kupata Kadi za Njano mbili na Wachezaji wao waliokuliwa na maumivu, Kiungo Sami Khedira, Arne Friedrich na Cacau, wote wako fiti.
Kocha wa Spain, Vicente del Bosque, itabidi afanye uamuzi mzito wa ama kumbakisha Fernando Torres au kumweka benchi kwa vile yuko chini ya kiwango.
Majeruhi wa Spain ni Cesc Fabregas na Carles Puyol ingawa wote wana nafasi kubwa ya kucheza.
Tathmini ya Mechi:
Hii ni Nusu Fainali ya 11 kwa Germany na safari hii ni Timu inayocheza staili tofauti na ya kuvutia kwa jinsi wanavyoonana Uwanjani na kushambulia kwa kasi.
Staili hiyo imeifanya Germany wazisage England bao 4-1 na kisha Argentina 4-0.
Spain iko tofauti mno na Spain inayojulikana na kila Mtu kwani safari hii inacheza Soka la kusuasua tofauti na lile Soka lao zuri lililozoeleka.
Hi ii mara ya kwanza kwa Spain, ambao ndio Mabingwa wa Ulaya, kufika Nusu Fainali ya Kombe la Dunia.
Historia kati ya Timu hizi mbili:
Katika mechi 8 za Miaka ya hivi karibuni, Spain wameifunga Germany mara mbili tu moja ikiwa ni Fainali ya Kombe la Mataifa ya Ulaya, EURO 2008.
Katika mechi 3 za Kombe la Dunia ambazo Nchi hizi zimekutana, Germany waliifunga Spain 2-1 Mwaka 1966 na pia kwa idadi hiyo hiyo ya magoli Mwaka 1982.
Huko USA Mwaka 1994, Germany na Spain zilitoka sare 1-1.
Nchi hizi zimekutana mara 20, Germany wakishinda mara 8, Spain mara 6 na sare 6.
Waamuzi:
Refa: Viktor Kassai (Hungary)
Wasaidizi: Gabor Eros naTibor Vamos (Wote toka Hungary)
Ujerumani kuipiku Brazil!!
Wakicheza mechi yao ya Nusu Fainali ya Kombe la Dunia Uwanja wa Moses Mabhida, Durban dhidi ya Spain Jumatano Julai 7, Germany watakuwa wanacheza mechi yao ya 98 kwenye Fainali za Kombe la Dunia tangu Kombe la Dunia lianzishwe Mwaka 1930 na hivyo kuipiku Brazil iliyocheza mechi 97.
Germany hawakuruhusiwa kucheza Fainali za Kombe la Dunia Mwaka 1950 kwa sababu ya matatizo yao ya kusababisha Vita Kuu ya Pili Duniani iliyomalizika Mwaka 1945.
Brazil ndio wanaonongoza kwa kuwa na rekodi nzuri kwa kucheza mechi 97, kushinda 67, sare 15 na kufungwa 15.
Ujerumani wameshinda 59, sare 19 na kufungwa 19.
Katika mechi hizo Brazil imefunga bao 211 na kufungwa 88 huku Germany ikiwa imefunga bao 203 na kufungwa 114.
Italy wamecheza jumla ya mechi 80, Argentina 70 na England 59.

Tuesday 6 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Holland yajikita Fainali!!!!
Holland 3 Uruguay 2
Holland imeipiga Uruguay bao 3-1 na kuingia Fainali za Kombe la Dunia katika mechi iliyochezwa Uwanja wa Green Park, Cape town.
Holland watakutana Fainali Siku ya Jumapili Uwanjani Soccer City, Soweto na Mshindi kati ya Germany na Spain.
Hii itakuwa ni Fainali ya 3 kwa Holland lakini katika mbili za Mwaka 1974
walifungwa na Germany na ile ya Mwaka 1978 walitolewa na Argentina.
Holland ndio waliopata bao mwanzo kwa shuti kali la mbali la Van Bronckhorst dakika ya 18.
Nae Diego Forlan akajibu mapigo kwa shuti la aina hiyo hiyo dakika ya 40.
Hadi mapumziko bao 1-1.
Kipindi cha pili, Holland wakapata bao mbili Wafungaji wakiwa Sneijder dakika ya 69 huku Van Persie akiwa wazi ofsaidi akimbabaisha Kipa na la tatu alifunga Arjen Robben dakika ya 72.
Kwenye dakika ya 90, Uruguay wakapata bao lao la pili kupitia Max Pereira.
Timu:
Uruguay: 1-Fernando Muslera; 3-Diego Godin, 6-Mauricio Victorino, 5-Walter Gargano, 16-Maximiliano Pereira, 22-Martin Caceres, 15-Diego Perez, 11-Alvaro Pereira, 17-Egidio Arevalo, 7-Edinson Cavani, 10-Diego Forlan.
Holland: 1-Maarten Stekelenburg; 12-Khalid Boulahrouz, 3-John Heitinga, 4-Joris Mathijsen, 5-Giovanni van Bronckhorst; 7-Dirk Kuyt, 6-Mark van Bommel, 10-Wesley Sneijder, 14-Demy de Zeeuw, 11-Arjen Robben; 9-Robin van Persie.
Refa: Ravshan Irmatov (Uzbekistan)
CHEKI: www.sokainbongo.com

Kocha mpya Ufaransa kujenga upya Les Bleus!!
Laurent Blanc, Miaka 44, amechukua wadhifa wa Kocha wa Ufaransa baada ya Raymond Domenech kumaliza Miaka 6 iliyoisha kwa fedheha na kuaibishwa huko Afrika Kusini walipotolewa Raundi ya Kwanza baada ya kushika mkia na pia Kikosi kukumbwa na ugomvi uliofanya Nicolas Anelka kutimuliwa.
Blanc, aliewahi kuwa Nahodha wa Ufaransa, amebainisha kuwa vitendo vilivyotokea huko Afrika Kusini vilimfedhehesha na ana nia kubwa ya kukutana na baadhi ya Wachezaji ili kuongea nao.
Mechi ya kwanza kwa Ufaransa chini ya Blanc itakuwa ni ile ya kirafiki dhidi ya Norway hapo Agosti 11 na kisha ni mechi ya mchujo ya EURO 2012 dhidi ya Balarus.
Blanc, aliewahi pia kuwa Difenda wa Manchester United, amekiri anahitaji bahati ili awe na mwanzo mwema kwa kuwa Timu haijakaa sawa na ina matatizo makubwa.
Pia amesema atakutana na Patrice Evra, aliekuwa Nahodha wa France huko Afrika Kusini, ambae Mchezaji wa Zamani wa France, Liliam Thuram, ametaka asiichezee tena Ufaransa kwa kuhusiana na mgomo huko Afrika Kusuni.
Mbali ya Evra, Blanc amesema atazungumza na Franck Ribery, Thierry Henry, William Gallas na Eric Abidal, ambao wote ndio wanaotuhumiwa kuchochea mgomo huko Afrika Kusini.
Man United kumchukua Sneijder?
Kuna uvumi mzito kuwa Manchester United huenda wakatoa ofa ya Pauni Milioni 30 kwa Inter Milan ili kumnunua Kiungo Wesley Sneijder, Miaka 26, ambae sasa anang’ara mno huko Afrika Kusini kwenye Kombe la Dunia na Nchi yake Uholanzi.
Sneijder, Mchezaji wa zamani wa Ajax na Real Madrid, alijiunga na Inter Milan Msimu uliokwisha baada ya kutemwa na Real na aliisaidia Inter, chini ya Jose Mourinho, kutwaa Ubingwa wa Ulaya.
Man United wanamchukulia Sneijder kama ni mrithi anaestahili kwa Kiungo wao Veterani, Paul Scholes, anaetegemewa kustaafu 2011.
Hata hivyo, Man United huenda wakapata upinzani mkubwa toka kwa Meneja mpya wa Inter Milan, Rafael Benitez, ambae huenda akagoma kumtoa Sneijder kwa Man United ambao ni Mahasimu wakubwa wa Klabu yake ya zamani Liverpool.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Fergie: Zigo la kutegemewa limemwelemea Rooney!!!
Sir Alex Ferguson amedai kuwa Wayne Rooney alishindwa kung’ara kwenye Fainali za Kombe la Dunia huko Afrika Kusini kwa sababu alielemewa na mzigo mzito wa kutegemewa na kila Mtu kuwa yeye ndie mkombozi wa England.
Ferguson, Meneja wa Manchester United, ambako Rooney aling’ara Msimu uliopita, amesema: “Nadhani matumaini makubwa ya kila Mtu yalimpa presha kubwa. Kila Mtu alidai Rooney ndie ataibeba England na atakuwa nyota kuliko Messi na Ronaldo. Watu wasubiri Fainali nyingine za Kombe la Dunia, baada ya Miaka minne Rooney ataibuka Mchezaji aliekomaa!”
Hata hivyo, Ferguson alionyeshwa kushangazwa na fomu ya England kwenye michuano hiyo ambayo walitolewa Raundi ya Pili walipopigwa 4-1 na Germany.
Lakini Ferguson amedai anaamini Germany wananufaika mno na kuwa na mapumziko ya Mwezi mmoja katikati ya Ligi yao Bundesliga ambayo huanza katikati ya Desemba hadi mwishoni Januari wakati ambao Ulaya hukumbwa na baridi kali.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Kitimtim leo: Holland v Uruguay
Macho ya Ulimwengu mzima yatakuwa Uwanja wa Green Park, Cape Town kushuhudia Nusu Fainali ya kwanza kati ya Holland na Uruguay.
Holland ilijikita Nusu Fainali hii baada ya kuwatoa Brazil bao 2-1 kwenye Robo Fainali baada ya kuwa nyuma 1-0 hadi mapumziko kwenye mechi hiyo.
Nao Uruguay wametinga hapa kwa msaada wa ujangili mkubwa wa Luis Suarez aliedaka mpira kwenye mstari wa goli dakika ya mwisho ya muda wa nyongeza wa dakika 30 na Ghana kupewa penalty ambyo Gyan Asamoah alipiga mwamba na kukosa kuipa ushindi Ghana na ndipo Uruguaya wakashinda kwa matuta 4-2.
Suarez, kwa uhalifu wake, alipewa Kadi Nyekundu na ataikosa mechi hii na nafasi yake itachukuliwa na Sebastian Abreu.
Mbali ya kumkosa Suarez, Kocha wa Uruguay, Oscar Tabarez, anakabiliwa na na kuumia kwa Wachezaji na pia kufungiwa kwa Jorge Fucile mechi moja.
Wachezaji wake majeruhi ni Nicolas Lodeiro, alievunjika mguu, na Diego Lugano.
Holland nao wanao Wachezaji wenye Kadi na hivyo kuikosa mechi hii na nao ni Gregory van der Wiel na Nigel de Jong.
Nafasi zao zinategemewa kujazwa na Khalid Boulhrouz na Demy de Zeeuw.
Mshindi wa mechi hii atacheza Fainali na Mshindi wa Argentina v Germany watakaocheza kesho.
Uruguay hawajaingia Fainali ya Kombe la Dunia tangu Mwaka 1950 walipowafunga Wenyeji Brazil 2-1 Uwanja wa Maracana na kutwaa Ubingwa wa Dunia kwa mara ya pili mara ya kwanza ilikuwa Mwaka 1930.
Holland wanawania kuingia Fainali yao ya 3, mara ya kwanza ilikuwa 1974 walipofungwa na Ujerumani nay a pili ilikuwa 1978 walipotolewa na Argentina.

Monday 5 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

Bundesliga kuanza Agosti 20
Mabingwa wa Ujerumani, Bayern Munich, wataanza kampeni yao ya kutetea Ubingwa wao wa Ligi ya Ujerumani, Bundesliga, wakiwa Uwanja wa nyumbani kwa kuivaa VfL Wolfsburg, waliokuwa Mabingwa 2009, hapo Agosti 20 wakati mechi za ufunguzi za Ligi zitakapoanza kuchezwa.
Msimu wa 2010/11 wa Bundesliga utamalizika Mei 14, 2011 na kutakuwa na mapumziko majira ya baridi kuanzia Desemba 19, 2010 hadi Januari 14, 2011.
Mechi nyingine Siku ya ufunguzi Agosti 20 ni ile ya Mshindi wa Pili, Schalke, atakaekuwa ugenini kucheza na SV Hamburg.
Timu iliyopanda Daraja St Pauli Hamburg itakuwa ugenini kuikwaa SC Freiburg na Cologne itaikaribisha Kaiserslautern.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Nigeria ‘Mikono Juu!’
Kuna taarifa kuwa Serikali ya Nigeria imefuta ile amri ya kuzuia Timu yake ya Taifa isicheze Soka la Kimataifa kwa Miaka miwili ikiwa ni saa moja tu kabla ule muda uliotolewa na FIFA wa kutaka amri hiyo ifutwe ufike na hivyo kukwepa kufungiwa na FIFA.
Amri hiyo ilitolewa baada ya Nigeria kutupwa nje ya Kombe la Dunia huko Afrika Kusini iliposhika mkia Kundi lake.
Jumapili, NFF, Chama cha Soka cha Nigeria, kiliwafukuza Rais wake na Makamu wake ili kuibembeleza Serikali iondoe amri yake ili kukwepa rungu la FIFA na inasemekana Kamati ya NFF leo ilikwenda kuonana na Rais wa Nigeria Goodluck Jonathan ili kumpigia magoti aifute amri yake.
CHEKI: www.sokainbongo.com

FIFA yatangaza Marefa wa Nusu Fainali
Kamati ya Marefa ya FIFA imetangaza Marefa watakaochezesha mechi za Nusu Fainali za Kombe la Dunia kati ya Uruguay v Holland na Germany v Spain zitakazochezwa Jumanne na Jumatano.
Refa wa Uruguay v Holland atakuwa ni Ravshan Irmatov kutoka Uzbekistan ambae ana Miaka 32 na ndie Refa mdogo kuchezesha mechi za Fainali za Kombe la Dunia tangu Mwaka 1934.
Refa Irmatov atasaidiwa na Rafael Ilyasov kutoka Uzbekistan na Bakhadyr Kochkarov kutoka Kazakhstan.
Mechi ya Germany v Spain itasimamiwa na Refa Viktor Kassai kutoka Hungary na atasaidiwa na wenzake kutoka Hungary, Gabor Eros na Tibor Vamos.
Mchezaji Bora Duniani kuwa na Tuzo moja tu!
Rais wa FIFA, Sepp Blatter, ametoboa kuwa kuanzia Mwakani Tuzo za Mchezaji Bora Duniani wa Mwaka wa FIFA na ile ya Ballon d’Or, yaani ‘Mpira wa Dhahabu’, zitaunganishwa na kuwa Tuzo moja tu.
Ballon d’Or ilianzishwa Mwaka 1956 na Gazeti la Ufaransa la Soka liitwalo ‘France Football’ na uteuzi wake wa Mchezaji Bora hufanywa na Wanahabari wa Soka wa Kimataifa na awali Washindi wake walikuwa ni Wachezaji wa Ulaya tu lakini baadae milango ikawa wazi kwa kila Mchezaji kuishinda.
Mwaka 2009, Lionel Mess indie alietwaa Ballon d’Or.
Mchezaji Bora Duniani wa Mwaka wa FIFA ilianzishwa Mwaka 1991 na Washindi huteuliwa na Makocha wa Timu za Taifa na Manahodha wao.
Mwaka 2009, Lionel Mess indie pia alitwaa Tuzo hii.
Tuzo hiyo moja mpya ya Mchezaji Bora Duniani wa Mwaka sasa itajulikana kama FIFA Ballon d’Or na itatolewa tarehe 10 Januari 2011 Mjini Zurich, Uswisi.
Jopo litalochagua Mshindi wa Tuzo hiyo mpya litakuwa ni mchanganyiko wa Waandishi wa Habari wa Kimataifa na Makocha wa Timu za Taifa na Makepteni.
Rio kupona kabla Ligi Kuu kuanza
Manchester United imetangaza kuwa Difenda wao Rio Ferdinand atapona goti aliloumia akiwa mazoezini na England huko Rustenburg, Afrka Kusini kabla kuanza kwa Kombe la Dunia na hivyo kuweza kucheza Ligi Kuu England itakayoanza Agosti 14.
Katika mechi ya kwanza ya Ligi Kuu Man United itacheza na Newcastle, Timu iliyopanda Daraja, Uwanjani Old Trafford.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Dunga atimuliwa Brazil
CBF, Chama cha Soka Brazil, kimemfukuza kazi Kocha wao Dunga kufuatia kutolewa kwenye Kombe la Dunia hatua ya Robo Fainali walipofungwa na Holland bao 2-1.
CBF imetamka kuwa Kocha mwingine atateuliwa kabla ya mwisho wa Mwezi wa Julai.
Dunga na Kikosi chake waliwasili Brazil kutoka Afrika Kusini siku ya Jumapili na mwenyewe alishatamka huo ndio mwisho wake na Timu ya Brazil.
Dunga alianza Ukocha na Timu ya Brazil Mwaka 2006 alipochukua nafasi hiyo toka kwa Carlos alberto Parreira ingawa hakuwa na sifa za Ukocha.
Dunga ndie aliekuwa Nahodha wa Brazil Mwaka 1994 walipotwaa Kombe la Dunia huko USA.
Brazil ndio watakuwa Wenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia Mwaka 2014.

Sunday 4 July 2010

CHEKI: www.sokainbongo.com

KOMBE LA DUNIA:
Kimbembe cha NUSU FAINALI!!
Kwa ufupi tu........:
Holland v Uruguay
Jumanne saa 3.30 usiku [bongo]
Uwanja wa Green Park, Cape Town,
Historia fupi:
Uruguay ni Nchi ya Watu Milioni 3.5, imeshinda Kombe la Dunia mara mbili, Miaka ya 1930 na 1950, na kufika Nusu Fainali mara 3, Miaka ya 1954, 1970 na 2010.
Holland ni Nchi pekee Duniani kufika Fainali za Kombe la Dunia mara mbili mfululizo, Mwaka 1974 na 1978, na kufungwa mechi zote za mwisho na kuambulia ushindi wa pili.
Uholanzi imefikia hatua ya Nusu Fainali mara mbili Mwaka 1998 na 2010.
Mategemeo:
Kocha wa Holland, Bert van Marwijk, ametamka: “Furaha za huko nyumbani Uholanzi ni kubwa!”
Mashabiki 20,000 wa Holland walioko Cape Town wataomba nderemo ziendelee.
Kocha wa Uruguay, Oscar Tabarez, amenena: “Uholanzi ndio wanaotegemewa kushinda! Ni ngumu kwetu lakini sio kitu kisichowezekana!”
Ufunguo wa mechi:
Timu zote ni ngumu kwenye Difensi.
Uholanzi imefungwa bao 3 katika mechi 5 na Uruguay mbili tu.
Mechi hii itataka ubunifu wa Wachezaji Mastaa wa Timu huku Holland wakimtegemea Wesley Sneijder na Uruguay Diego Forlan kuifungua mechi hii.
Uteuzi wa Wachezaji:
Holland itamkosa Kiungo Mlinzi Nigel de Jong anaetumikia kifungo cha mechi moja na nafasi yake itachukuliwa na Stijn Schaars ingawa hata Rafael van der Vaart, kawaida ni Kiungo Mshambuliaji, anaweza kucheza.
Uruguay watamkosa Luis Suarez aliefungiwa mechi moja kwa kuleta ujangili mechi ya Ghana kwa kile alichokiita ‘Mkono wa Mungu’ na nafasi yake itazibwa na Sebastian Abreu.
Germany v Spain:
Jumanne saa 3.30 usiku [bongo]
Uwanja wa Moses Mabhida, Durban
Historia fupi:
Spain wana historia mbovu kwenye Kombe la Dunia.
Nafasi bora Spain waliyoweza kufika ni nafasi ya 4 Mwaka 1950 na hii ni mara ya kwanza kuingia Nusu Fainali.
Germany wao ni Mabingwa wa Dunia mara 3 na hii ni mara yao ya 12 kutinga Nusu Fainali.
Mategemeo:
David Villa, Mchezaji wa Spain anaeongoza kwa kupachika bao 5 kwenye Fainali hizi, anajipa matumaini: “Mpinzani kama Germany ndie anatupa changamoto kubwa na si Paraguay tulipocheza ovyo tu!”
Mashine ya Kijerumani ya Wachezaji Vijana zaidi wako watulivu bila mchecheto.
Ufunguo wa mechi:
Hii itakuwa mechi ambayo ushindi utapatikana kwa yule atakaetawala Kiungo.
Bila shaka, Xavi wa Spain na ile injini ya Ujerumani Bastian Schweinsteiger ndio watakaobeba Timu zao.
Uteuzi wa Wachezaji:
Kocha wa Ujerumani Joachim Low atalazimika kumbadilisha Thomas Muller na kumchezesha Piotr Trochowski kwa vile Muller amefungiwa mechi moja.
Spain wao, wakifanya badiliko lolote, itakuwa ni kimbinu tu kwani hawana majeruhi wala aliefungiwa na kuna minong’ono Fernando Torres, ambae kiwango kipo chini, huenda akabadilishwa na Llorente.
CHEKI: www.sokainbongo.com

Nyota 5 hazikung’ara!!!
Huko Afrika Kusini kwenye Fainali za Kombe la Dunia, kila mtu alitegemea ndio jukwaa bora kwa Wachezaji Bora duniani kung’ara na kuwika.
Nyota 5 zilizotegemewa kung’ara huko bondeni ni Lionel Messi, Cristiano Ronaldo, Wayne Rooney, Kaka na Didier Drogba lakini, baada ya jana Argentina kupokea kipondo cha 4-0 toka kwa Germany, wote hao wamerudi makwao mapema, mikono mitupu na bila kung’ara.
Kati yao Mastaa hao watano, ni wawili tu, Drogba na Ronaldo, ndio walioweza kutingisha nyavu tena ni bao moja moja tu na wote, kwa ujumla, hawakung’ara kabisa na zile cheche zao zilionekana kwa vipindi vifupi tu kama moto uliokuwa unataka kuzimika.
Wadau wamebaki wanakuna vichwa kujiuliza kulikoni?
Lakini, pengine, jibu sahihi limetoka kwa Mtu ambae aliwahi kutamba kuwa ni Bora miongoni mwa Bora wote, Diego Armando Maradona, ambae alihojiwa nini kimewasibu Messi, Rooney na Ronaldo, na akajibu: “Ni gemu tufauti siku hizi. Enzi zetu tulikuwa Wachezaji wachoyo! Mie, nilitaka kufanya kila kitu peke yangu kwenye Timu ndani ya mchezo! Lakini siku hizi, Rooney na Messi, wanajiona kuwa Timu ikiwahitaji ndani ya mchezo ni wajibu wao kucheza kwa ajili ya Timu!”
Inawezekana ni kweli kwani siku hizi ni Mchezo wa Kitimu badala ya Ubinafsi wa Mchezaji!
Mfano hai na sahihi huko Bondeni ni Timu ya Ujerumani isiyokuwa na Supastaa lakini ni hatari mno kama Timu!
Hiyo ndiyo Mashine ya Kijerumani!
CHEKI: www.sokainbongo.com

Nigeria watimuana!
NFF, Chama cha Soka cha Nigeria, kimewatimua Viongozi wawili ambao ni Rais wa NFF na Makamu wake ili kumbembeleza Rais wa Nchi yao, Goodluck Jonathan, abadilishe msimamo wa kuizuia Nchi hiyo kucheza Mashindano ya Kimataifa kwa Miaka miwili na hivyo kukwepa adhabu ya kusimamishwa na FIFA kwa kuingiliwa na Serikali.
FIFA imeipa Nigeria mpaka Jumatatu jioni Julai 5 ili iondoe uamuzi wa kuizuia kucheza Kimataifa la sivyo itachukuliwa hatua.
Hodgson ahofia kufa urafiki na Fergie
Meneja mpya wa Liverpool, Roy Hodgson, ana wasiwasi kujiunga kwake na Liverpool kutatia doa uhusiano wake na rafiki yake Sir Alex Ferguson, Meneja wa Manchester United.
Liverpool na Manchester United ni Klabu Mahasimu na wapinzani wakubwa sana huko England.
Hodgson amesema: “Najua Sir Alex si mtu wa Liverpool hivyo nina wasiwasi uhusiano wetu utaharibika! Lakini itabidi niongee nae na tunywe mvinyo pamoja hata kwa siri!”
CHEKI: www.sokainbongo.com

Spain yajikongoja kuingia Nusu Fainali
Spain 1 Paraguay 0
David Villa amefunga bao lake la 5 kwenye Kombe la Dunia huko Afrika Kusini na kuwa ndie aneongoza kwa ufungaji na pia kuiingiza Spain kwenye Nusu Fainali kukutana na Germany.
Villa alifunga bao lake dakika ya 82.
Awali Nelson Valdez wa Paraguay alifunga bao safi lakini lilikataliwa kwa kile kilichodaiwa ni ofsaidi.
Mechi hii ilishuhudia penalti 3 na zote hazikuzaa bao.
Penalti ya kwanza walipewa Paraguay baada ya Refa Carlos Batres toka Guatemala kumwona Gerard Pique akimwangusha Cardozo lakini Cardozo akakosa penalti hiyo baada ya Kipa Casillas kuokoa.
Dakika mbili baadae ikaja zamu ya Spain wakati Alcaraz alipomvaa Villa na Alonso akapiga penalti na kufunga lakini Refa akadai Spain waliingia ndani ya boksi kabla kupigwa na hivyo irudiwe.
Alonso akarudia hiyo penalti na Kipa Villar akaokoa.
Ndipo ikafika dakika ya 82 na likazaliwa goli la ushindi na la kushangaza kwa vituko vyake.
Iniesta alichanja mbuga na angeweza kufunga mwenyewe lakini bila uchoyo akampasia Pedro ambae shuti lake liligonga mwamba na kurudi.
Villa akaunasa mpira huo uliorudi na akaupiga ukagonga posti moja na kwenda kugonga ya pili na kisha kutiririka kuingia wavuni.
Kwa ujumla Spain walicheza mechi hii chini ya kiwango na ikiwa watataka kuifunga Germany mechi ijayo ni lazima wabadilike au Mashine ya Kijerumane itasaga tena Mtu.
Powered By Blogger