Saturday 5 June 2010

Mastaa wazidi kupukutika Kombe la Dunia!!
Walianza Ballack, Essien, Rio na sasa Mikel huku Drogba…………….!
Kiungo wa Nigeria, John Mikel Obi, hatacheza Kombe la Dunia baada ya kuthibitika goti lake alilokuwa akiliuguza halitapona mapema.
Mikel anaungana na Mastaa wengine wa Klabu yake Chelsea, kina Ballack, Michael Essien na huenda pia Drogba, kuwa nje ya Kombe la Dunia baada ya kuumia.
Mikel alifanyiwa operesheni ndogo ya goti Mwezi Mei na inasemekana hajapona vizuri.
Msemaji wa Timu ya Nigeria amesema imebidi wamwache baada ya mwenyewe Mikel kujiona hajapona vizuri na kuendelea kuwepo na Nigeria kungesababisha kupata athari zaidi.
Nafasi ya Mikel imechukuliwa na Brown Ideye ambae ni Straika kutoka Klabu ya Ufaransa Sochaux na Ideye hajawahi kuichezea Nigeria hata mara moja.
Nigeria wapo Kundi B pamoja na Argentina, Ugiriki na Korea Kusini na watacheza mechi yao ya kwanza Juni 12 dhidi ya Argentina.
PATA MAMBO MAPYA MOTO: www.sokainbongo.com

Elton John afanya tamasha kuisaidia Watford
Gwiji la Muziki, Elton John, ambae aliwahi kuwa Mmiliki na pia Mwenyekiti wa Klabu ya Watford inayocheza Ligi Daraja la Coca Cola Championship, amefanya Tamasha maalum kuisaidia Watford kununua Wachezaji.
Tamasha hilo llifanyika Jumamosi iliyopita Uwanja wa Klabu hiyo uitwao Vicarage Road na llilingiza Pauni 600,000.
Elton John alikuwa Mmiliki na Mwenyekiti wa Watford kati ya Mwaka 1976 na 1987.
Pia, Mwaka 2005 aliwahi kufanya Tamasha kama hilo kuchangia Watford.
Rio anahisi kalaanika!!
Nahodha wa England, Rio Ferdinand, ambae jana aliumia goti mazoezini huko Rusternburg, Afrika Kusini na hivyo kulikosa Kombe la Dunia linaloanza Juni 11, anahisi kama ‘amelaanika’ kwa kuumia huko.
Uchunguzi katika Hospitali moja huko Rusternburg umebaini kuwa anahitaji Wiki 4 hadi 6 ili kupona goti hilo.
Mkasa huo kwa Rio unafuatia Msimu mzima wa Mwaka 2009/10 ulioisha Mei 9 ambao amekuwa akiandamwa na kuumia mara kwa mara kulikomfanya aichezee Klabu yake Manchester United Mechi 13 tu za Ligi Kuu.
Wakala wa Rio Ferdinand, Pini Zahavi, amesema Mteja wake amemwambia anahisi kama ‘amelaanika’ kwani haelewi kwa nini hilo limetokea.
Hata hivyo, Zahavi amesisitiza Rio, mwenye Miaka 31, ni Mtu imara na si ajabu akaibuka na kuichezea England Fainali za Kombe la Dunia Mwaka 2014 huko Brazil.
Essien aongeza Mkataba Chelsea
Michael Essien ameongeza nyongeza ya Miaka miwili katika Mkataba wake na Chelsea na atabaki Klabu hiyo hadi 2015.
Essien alijiunga na Chelsea Mwaka 2005 akitokea Lyon ya Ufaransa na ameshaichezea Klabu hiyo ya Stamford Bridge mechi 185 na kufunga mabao 22.
Kwa sasa Essien, Miaka 27, anauguza goti alililoumia katikati ya Msimu uliokwisha juzi wa Mwaka 2009/10 na maumivu hayo yamemfanya akose nusu ya pili ya Msimu wa Ligi Kuu England na pia ameshindwa kuichezea Ghana kwenye Fainali za Kombe la Dunia linaloanza Juni 11 huko Afrika Kusini ambapo Ghana ipo Kundi D pamoja na Ujerumani, Serbia na Australia.
Barca bado wana Fabregas!!
Rais wa Barcelona, Joan Laporta, bado ana imani kubwa Arsenal watamruhusu Cesc Fabregas ahamie kwao licha ya Ze Gunners kuipangua ofa yao wiki iliyopita.
Fabregas, mwenye Mkataba na Arsenal hadi 2015, ameshataja nia yake kurudi Barca alikoanzia kucheza Soka akiwa mtoto.
Inasemekana Arsenal waliikataa ofa ya Barca ya kumnunua Fabregas kwa Pauni Milioni 29 na Laporta amesema: “Hiyo ndiyo bei tunayoona ni thamani yake. Arsenal wameikataa na sasa ni juu yetu kuamua hatua inayofuata. Tunaongea nao.”
Laporta aliongeza kuwa wao walitaka wakubaliane na Arsenal kabla kuanza kwa Kombe la Dunia lakini wao hawana wasiwasi na wataendelea kuongea na Arsenal.
Kisu kumuokoa Drogba acheze Bondeni
Ushiriki wa Nahodha wa Ivory Coast Didier Drogba Fainali za Kombe la Dunia huenda ukaokolewa kwa kufanyiwa operesheni ili kuunga mfupa uliovunjika kwenye kiwiko cha mkono wake wa kulia na baada ya upasuaji huo atahitaji siku 10 kupona.
Drogba aliumizwa jana alipovaana na Sentahafu wa Japan, Marcus Tulio Tanaka, mzaliwa wa Brazil, katika mechi ya kirafiki huko Uswisi ambayo Ivory Coast walishinda 2-0.
Kocha wa Ivory Coast, Sven-Goran Eriksson, amesema bado ipo nafasi kwa Drogba kucheza Fainali za Kombe la Dunia zinazoanza huko Africa Kusini Juni 11 na mechi ya kwanza kwa Ivory Coast ni Juni 15 dhidi ya Ureno.
Ivory Coast wapo Kundi G pamoja na Brazil, Ureno na Korea Kaskazini.
Eriksson alisema: “Huenda akafanyiwa operesheni na huenda akacheza Fainali. Amevunjika mfupa karibu na kiwiko lakini atamwona Speshelisti. Tutajua kesho!”
Drogba ndie Mfungaji Bora wa Ligi Kuu England kwa Msimu ulioisha hivi karibuni wa Mwaka 2009/10.
RATIBA MECHI ZA KIRAFIKI ZA KIMATAIFA
Jumamosi, Juni 5
Holland v Hungary
South Africa v Denmark
Australia v USA
Ghana v Latvia
Slovakia v Costa Rica
Algeria v UAE
Romania v Honduras
Serbia v Cameroon
Switzerland v Italy

Friday 4 June 2010

MATOKEO MECHI ZA LEO ZA KIMATAIFA ZA KIRAFIKI
Ijumaa, Juni 4
Ivory Coast 2 v Japan 0 [Marcus Tulio Tanaka, kajifunga dak 13, Yaya Toure, dak 79]
France 0 v China 1 [Deng Zhuoxiang, dak 68]
Slovenia 3 v New Zealand 1 ]
Rio nje Kombe la Dunia
Nahodha wa England, Rio Ferdinand, hatacheza Kombe la Dunia baada ya kuumizwa goti lake la mguu wa kushoto leo mazoezini huko Rustenburg, Afrika Kusini.
Inasemekana Rio aliumizwa goti hilo baada ya kuvaana na Emile Heskey kwenye mazoezi.
England imemwita Beki wa Tottenham, Michael Dawson, kuchukua nafasi ya Rio Ferdinand.
Dawson alikuwemo kwenye Kikosi cha awali cha Wachezaji 30 lakini aliachwa Siku ya Jumanne baada ya Kikosi hicho kupunguzwa na kuwa Wachezaji 23 wa mwisho.
Sasa Unahodha atachukua Steven Gerrard ambae alikuwa Naibu wa Rio.
Kombe la Dunia kwa Drogba ni hatihati!!
Nahodha wa Ivory Coast, Didier Drogba, huenda akalikosa Kombe la Dunia kufuatia kuvunjika kwa kiwiko chake cha mkono wa kulia.
Drogba aliumizwa kwenye mechi ya kirafiki leo huko Switzerland walipocheza na Japan ambayo Ivory Coast walishinda 2-0 alipogongana na Beki wa Japan Marcus Tulio Tanaka.
Ingawa kulikosa Kombe la Dunia hakujathibitishwa na Viongozi wa Ivory Coast lakini Beki wa Timu hiyo anaichezea Manchester City, Kolo Toure, amedai Drogba hawezi kucheza Fainali hizo na ameambiwa hilo na mwenyewe Drogba.
Hata hivyo mpaka sasa habari hizo hazijathibitishwa.
Liverpool waanza msako wa Meneja mpya
Baada ya kupeana mkono wa kwaheri kufuatia makubaliano ya pamoja na Rafael Benitez, Liverpool inaanza msako wa kumpata Meneja mpya na jukumu hilo limetundikwa kwa Mkurugenzi Mkuu, Christian Purslow, na Kenny Daglish, ambae aliwahi kuwa Meneja wa Liverpool hapo zamani na sasa ni Balozi wa Chuo cha Soka Klabuni humo.
Majina ya Warithi yanayotajwa ni Roy Hodgson wa Fulham, Martin O’Neill wa Aston Villa na Mark Hughes, Meneja wa zamani wa Manchester City.
Lakini baadhi ya Wachezaji wa zamani wa Liverpool, wakiwemo Kipa kutoka Zimbabwe, Bruce Grobbelaar, na Jamie Redknapp, wanataka Kenny Daglish ashike hatamu.
Baba aacha kazi ende Bondeni kumwona Mwanawe Chicharito!!
Baba Mzazi wa Mchezaji mpya wa Manchester United, Javier ‘Chicharito’ Hernandez, anaechezea Timu ya Mexico ambayo imo kwenye Fainali za Kombe la Dunia zitakazoanza Afrika Kusini Juni 11, ameamua kuacha kazi yake ili asafiri kwenda Afrika Kusini kumshuhudia Mwanawe akicheza Fainali hizo.
Baba huyo, Hernandez, ni Meneja wa Timu ya Rezevu ya Klabu ya Chivas ya huko Mexico, ambao ni vigogo huko, aliomba ruhusa lakini akanyimwa na ndipo alipoamua kuacha kazi.
Baba huyo wa Chicharito amesema: “Niliomba ruhusa nikatizame Kombe la Dunia wakakataa. Nikakaa chini na Familia yangu na tukaamua niache kazi ili niende Afrika Kusini kumwona Mwanangu akicheza. Kwa hilo, kazi si muhimu. Ni uamuzi mzito lakini lazima ujue hapa Duniani hatuishi milele. Waajiri wapo milele, lakini mtu huko milele.”
Janja ya Korea Kaskazini, FIFA Gundua!!!!!
Korea Kaskazini walitua Afrika Kusini wakiwa na Straika mmoja akitajwa kama Kipa wao wa tatu kama FIFA inavyotaka kwamba Listi ya Wachezaji 32 kwa Nchi zote zilizo Fainali ya Kombe la Dunia ziwe na Makipa watatu lakini mpango huo umepigwa chini na FIFA.
FIFA imewaambia Korea Kaskazini kuwa Mchezaji Kim Myong-won, ambae kawaida ni Straika, ataruhusiwa kucheza kama Kipa tu kwenye Fainali za Kombe la Dunia kwa vile jina lake limesilishwa kwao kuwa ni Kipa katika Listi ya mwisho ya Wachezaji 32 ambazo Nchi zote zilizoko Fainali Kombe la Dunia zilitakiwa kuwasilisha Juni 1.
Kocha wa Korea Kaskazini, Kim Jong-hun, alitangaza Majina ya Makipa wawili tu na kumtaja Straika Kim kuwa ni Kipa wa Tatu.
Korea Kaskazini wako Kundi G pamoja na Brazil, Ivory Coast na Ureno.
FIFA imetoa stetimenti kuelezea hali hiyo ya Korea Kaskazini na imesema: “Listi za Wachezaji 32 kwa kila Timu zilizowasilishwa kwetu Juni 1 ni za mwisho na haziwezi kubadilishwa. Listi hiyo ya Wachezaji 32 inataka Makipa wawe watatu. Kitu pekee kinachoweza kubadili listi hizo ni endapo Mchezaji ataumia vibaya Masaa 24 kabla ya Mechi ya kwanza, Mchezaji huyo anaweza kubadilishwa. Wachezaji watatu waliotajwa kama Makipa wanaruhusiwa kucheza nafasi ya Kipa tu kwenye Fainali hizi za Kombe la Dunia na hili limetangazwa kwa kila Timu. Hivyo Kim Myong-won haruhusiwi kucheza kama Straika.”
MATOKEO MECHI ZA KIMATAIFA ZA KIRAFIKI
Alhamisi, Juni 3
Spain 1 v Korea Kusini 0 [Mfungaji Jesus Navas, dak ya 85]
Italy 1 v Mexico 2
-Mexico [Vela, 17 Medina, 83]
-Italia [Bonucci, 89]
Germany 3 v Bosnia and Herzegovina 1
-Ujerumani [Phillip Lahm, 50, Schweinsteiger, 73 na 77, zote penalti]
-Bosnia [Edin Dzeko, 15]
RATIBA MECHI ZA LEO: Ijumaa, Juni 4
Ivory Coast v Japan
France v China
Slovenia v New Zealand

Thursday 3 June 2010

Benitez ang’oka Liverpool!!
Liverpool imethibitisha kuwa Rafa Benitez, ambae amedumu kwa Miaka 6, ataondoka Klabuni hapo baada ya makubaliano ya pande zote.
Baada ya Msimu mbovu uliokwisha Mwezi Mei, Benitez alijikuta yupo mashakani Timu ilipomaliza nafasi ya 7 kwenye Ligi Kuu na hivyo kuikosa nafasi ya kucheza UEFA CHAMPIONS LIGI Msimu ujao.
Uhusiano wa Benitez na Wamiliki wa Klabu hiyo, Wamarekani wawili Tom Hicks na George Gillet, ulikuwa mbaya na walikuwa hawasikilizani.
Katika kipindi chake cha Miaka 6 hapo Liverpool, Benitez alifanikiwa kunyakua Klabu Bingwa Ulaya Mwaka 2005 na FA Cup Mwaka uliofuata lakini tangu wakati huo Liverpool imekuwa ikiambua patupu kila Msimu.
Akizungumza kwenye tovuti ya Liverpool, Benitez alitamka: “Nimesikitika sana kwamba mie si Meneja tena wa Liverpool na natoa shukrani zangu kwa Wafanyakazi na Wachezaji wote. Daima ntayaweka mema yote moyoni pamoja na mapenzi ya Washabiki. Sina maneno ya kusema ya kuwashukuru na ninajisikia fahari mno kusema nilikuwa Meneja wenu. Ahsanteni sana na daima kumbukeni: “Hamtatembea peke yenu!”
Kuondoka kwa Benitez kumezua utata kuhusu hatma ya Wachezaji Mastaa kama vile Nahodha wao Steven Gerrard, Fernando Torres na Javier Mascherano ambao wote wamekumbwa na uvumi mkubwa kuwa sasa milango yao ya kuondoka iko wazi.
Mbali ya utata wa Wachezaji kuondoka, pia haijajulikana nani atakuwa Mrithi wa Benitez hasa ukitilia maanani hata umiliki wa Klabu hiyo uko mashakani kwa vile wenye mali, Tom Hicks na George Gillet, wamekuwa kwa muda mrefu wakitafuta mnunuzi jambo ambalo limekuwa gumu kwa vile Klabu ina madeni makubwa.
Benitez mguu nje Anfield
Meneja wa Liverpool Rafael Benitez yupo njiani kuondoka hapo Anfield baada ya uongozi wa Klabu kumpa ofa ya Pauni Milioni 3 ili aende zake.
Benitez alisaini Mkataba wa Miaka mitano Mwaka 2009 lakini hamna mafanikio yeyote yaliyopatikana huku Klabu ikiwa inaandamwa na Madeni ya zaidi ya Pauni Milioni 350.
Wamiliki wa Liverpool, Wamarekani wawili, Tom Hicks na George Gillet, wamekuwa wakitafuta mnunuzi bila mafanikio.
Habari toka ndani ya Klabu hiyo zimesema upo uhakika Benitez ataondoka Klabuni hapo wikiendi hii huku Inter Milan ikitajwa kuwa ndiko aendako kuchukua nafasi ya Jose Mourinho aliehamia Real Madrid.
Liverpool inasemekana inataka kumuondoa Benitez kwa kumpa ofa hiyo ili kukwepa kumlipa Pauni Milioni 16 ikitaka kumtimua kabla ya Mkataba wake kumalizika.
Grant athibitishwa Meneja West Ham
Avram Grant amethibitishwa kama Meneja mpya wa West Ham na amepewa Mkataba wa Miaka Minne.
Grant anachukua nafasi ya Gianfranco Zola alietimuliwa.
Grant amekaririwa akisema anasikia fahari kwa kuteuliwa Meneja wa West Ham.
Wachezaji England wapewa namba zao za Jezi
Kocha wa England, Fabio Capello, ametangaza namba za Jezi za Wachezaji wake 23 wa Fainali za Kombe la Dunia huku Joe Cole, David James na Peter Crouch wakiwa ndani ya Listi ya Wachezaji 11 wa kwanza.
Kipa David James amepewa Jezi namba 1, Crouch namba 9 na Joe Cole namba 11.
Ingawa nambari za Jezi si kigezo cha kuwa Wachezaji hao ndio wapo Timu ya Kwanza, lakini Wataalam wanahisi hicho ni kipimo tosha cha kuonyesha Wachezaji gani wapo mbele katika uteuzi.
Nahodha wa England, Rio Ferdinand, ametamka: “Hakuna Mchezaji alie salama. Meneja huyu haogopi kuwabwaga Wachezaji wenye sifa akiwaona hawachezi vizuri. Yeye anashughulikia kila kitu vizuri tu.”
England watacheza mechi yao ya kwanza ya Kombe la Dunia Juni 12 dhidi ya USA Uwanja wa Royal Bafokeng Mjini Rustenburg.
Timu hiyo ilitua Johannesburg leo asubuhi ikitokea London na ilienda moja kwa moja Kambini kwao Kituo cha Michezo cha Royal Bafokeng kilichopo Rustenburg.
Kikosi kamili cha England na Namba za Jezi:
1. David James
2. Glen Johnson
3. Ashley Cole
4. Steven Gerrard
5. Rio Ferdinand
6. John Terry
7. Aaron Lennon
8. Frank Lampard
9. Peter Crouch
10. Wayne Rooney
11. Joe Cole
12. Robert Green
13. Stephen Warnock
14. Gareth Barry
15. Matthew Upson
16. James Milner
17. Shaun Wright-Phillips
18. Jamie Carragher
19. Jermain Defoe
20. Ledley King
21. Emile Heskey
22. Michael Carrick
23. Joe Hart
MATOKEO MECHI ZA KIRAFIKI LEO:
Jumatano, Juni2
Zimbabwe 0 v Brazil 3
Ugiriki 0 v Paraguay 2
Azerbaijan 0 v Honduras 0
Romania 0 v Macedonia 1
Norway 0 v Ukraine 1
Belarus 0 v Sweden 1
Albania 1 v Andorra 0
Serbia 0 v Poland 0
MECHI ZA LEO ZA KIMATAIFA ZA KIRAFIKI
Alhamisi, Juni 3
Spain v Korea Kusini [saa 1 usiku]
Italy v Mexico [saa 2 na robo usiku]
Germany v Bosnia and Herzegovina [saa 3 na nusu usiku]

Wednesday 2 June 2010

Capello na Mkataba mpya!
Wakati England leo ipo njiani kwenda Bondeni kwa ajili ya Fainali za Kombe la Dunia, Meneja wao, Fabio Capello, amesaini Mkataba mwingine ambao una marekebisho yaliyoondoa kipengele cha kuruhusu yoyote kati ya pande mbili, yaani upande wa Capello na upande wa FA England, kuvunja Mkataba kabla ya muda wake kwisha hapo Mwaka 2012.
Marekebisho hayo sasa yatamfanya Capello abaki Kocha wa England hadi baada ya Fainali za EURO 2012 na hivyo kuondoa ile minong’ono kuwa yuko mbioni kwenda kumrithi Jose Mourinho huko Inter Milan mara tu baada ya Fainali za Kombe la Dunia.
Capello mwenyewe alikuwa amewaonya Wachezaji wake wa England wasiingize hatma zao za uhamisho toka Klabu zao wakati wapo kambini na England na hivyo kuathiri morali, kwa hivyo kwa yeye binafsi kusaini Mkataba mwingine kumeondoa kiwingu kichwani mwake.
Marekebisho hayo ya Mkataba pia yamethibitishwa na FA.
Boateng kuhamia Man City!
Beki wa Ujerumani, Jerome Boateng, ambae ni nduguye Kevin-Prince Boateng aliepata sifa mbaya ya kumng’oa Nahodha wa Ujerumani, Michael Ballack, toka Kombe la Dunia baada ya kumuumiza, amesema atasaini Manchester City kabla ya kuanza za Fainali za Kombe la Dunia ambalo yeye ni mmoja wa Wachezaji wa Timu ya Taifa ya Ujerumani.
Boateng, mwenye miaka 21, na anaechezea Bundesliga na Klabu ya Hamburg, amethibitisha Kocha wa Man City, Roberto Mancini, alimfuata Hamburg na amemfanya akubali kuchezea Man City.
Boateng amesema amelazimika kuondoka Ujerumani baada ya Familia yao kuandamwa na Wanahabari baada ya nduguye kumuumiza Ballack kwenye Fainali ya FA CupChelsea ilipocheza na Portsmouth na hivyo kumfanya ashindwe kucheza Kombe la Dunia.
Jerome Boateng huenda akakumbana na Kevin-Prince Boateng kwenye Kombe la Dunia baada ya Kevin-Prince kuamua kuichezea Ghana, ambayo ni Nchi ya Baba yake, kwa vile Ujerumani na Ghana zipo Kundi D pamoja.
Jerome Boateng amelalamika: “Inanisumbua jinsi Familia yetu inavyoandamwa! Nyumbani kwetu mlangoni wamejazana Wapiga Picha na hatuwezi hata kutoka nje! Nimejaribu kuwaita Polisi lakini wanasema hawana la kufanya na inabidi tuikubali hali kwa vile sisi ni Boateng! Hii imefika mbali!”
Zimbabwe 0 Brazil 3
Leo huko Harare, Zimbabwe, Uwanja wa Taifa, Brazil ambayo ipo Afrika Kusini kwa ajili ya Fainali za Kombe la Dunia, imeichapa Zimbabwe bao 3-0 katika mechi ya kirafiki.
Hadi mapumziko, Brazil ilikuwa mbele kwa bao 2-0 wafungaji wakiwa Bastos dakika ya 42 na Robinho dakika ya 44.
Elano aliongeza bao la 3 kwenye dakika ya 56.
Brazil watasafiri kwenda Dar es Salaam, Tanzania kucheza na Taifa Stars, Timu ya Taifa ya Tanzania, hapo Jumatatu Juni 7.
Brazil wapo Kundi G kwenye Fainali za Kombe la Dunia pamoja na Korea Kaskazini, Ivory Coast na Ureno.
Brazil watacheza mechi yao ya kwanza Juni 15 dhidi ya Korea Kaskazini.
Ze Gunners waikataa ofa ya Barca kwa Fabregas!!
Arsenal wamekataa kusikiliza ofa ya FC Barcelona ya kutaka kumnunua Nahodha wao Cesc Fabregas na wamesisitiza wao hawana nia ya kumhamisha Mchezaji huyo wa Kimataifa wa Spain alie njiani kwenda kwenye Fainali za Kombe la Dunia na Nchi yake.
Inadaiwa Barcelona waliwasilisha ofa rasmi ya kumnunua Fabregas hapo juzi.
Fabregas, miaka 23, alizungumza wiki iliyopita na kudai kuwa yupo na nia ya kurudi Barcelona alikoanzia Soka lake akiwa mtoto.
Arsenal imeikataa ofa hiyo ya Barcelona na imetangaza kwenye tovuti ya Klabu hiyo kwamba Mchezaji huyo ana Mkataba hadi 2015 na ni muhimu na anathaminiwa sana na Ze Gunners.
Grant kutua West Ham
Bosi wa zamani wa Portsmouth na Chelsea Avram Grant huenda leo akatangazwa Meneja mpya wa West Ham kuchukua nafasi ya Gianfranco Zola aliefukuzwa.
Grant aliondoka Portsmouth, Timu iliyoshushwa Daraja, hapo Mei 21 na inasemekana amekatiza vakesheni yake ili aende London kukamilisha taratibu za kutua West Ham.
Wamiliki wa pamoja wa West Ham, David Sullivan na David Gold, wamekubaliana kuhusu uteuzi wa Grant ambae alipokuwa Chelsea aliiwezesha kufika Fainali ya UEFA CHAMPIONS LIGI lakini ikabwagwa na Manchester United na pia aliifikisha Portsmouth Fainali ya FA Cup lakini ikafungwa na Chelsea.
‘WAKOMBOZI WEKUNDU’ wabwaga manyanga Man United!!!
Kile Kikundi cha Mashabiki Matajiri waliokubuhu wa Manchester United, maarufu kama ‘Wakombozi Wekundu’, waliokuwa na nia ya kuinunua Man United kutoka kwa Wamiliki wake, Familia ya Kimarekani ya Glazer, wamesimamisha azma yao ya kutoa ofa ya ununuzi wa Klabu hiyo.
Kundi hilo limedai thamani ya Klabu hiyo imepotoshwa mno na Vyombo vya Habari na azma yao pia imepindishwa na hivyo kulifanya zoezi lao lipata upinzani.
Wiki iliyopita, Familia ya Glazer, ilitangaza kuwa hawana nia ya kuiuza Manchester United ambayo waliinunua Mwaka 2005 kwa Pauni Milioni 800.
Mbali ya Kundi hilo la Matajiri, ‘Wakombozi Wekundu’, Familia hiyo ya Glazer imekuwa ikipingwa na Kundi la Mashabiki wanaojiita MUST [The Manchester United Supporters Trust] waliokuwa wakiendesha kampeni kwa kuwataka wafuasi wao wavae sare za rangi ya Kijani na Dhahabu hizo zikiwa ndizo rangi za Klabu anzilishi ya Man United, Newton Heath, iliyoanzishwa Mwaka 1878 na Wafanyakazi wa Depo ya Reli.
KILA NCHI YAWASILISHA VIKOSI VYA WACHEZAJI 23 FIFA!!
SOMA ZAIDI MAJINA YA VIKOSI VYA NCHI ZOTE 32 FAINALI ZA KOMBE LA
DUNIA
BOFYA HAPA
MATOKEO MECHI ZA KIRAFIKI ZA MATAIFA:
Jumanne, 1 Juni 2010
Australia 1 v Denmark 0
Netherlands 4 v Ghana 1
Portugal 3 v Cameroon 1
Switzerland 0 v Costa Rica 1

Tuesday 1 June 2010

Kikosi cha ENGLAND Kombe la Dunia chatajwa!!!
• Leighton Baines, Michael Dawson, Tom Huddlestone, Scott Parker, Adam Johnson, Theo Walcott & Darren Bent NJE!!!!.
Hatimaye Fabio Capello ametangaza Kikosi chake cha Wachezaji 23 ambao atasafiri nao hapo kesho kwenda Afrika Kusini tayari kwa Fainali za Kombe la Dunia linaloanza Juni 11.
Majina hayo ya Wachezaji 23 yanatakiwa yafikishwe FIFA leo.
Wachezaji waliotolewa na kuachwa toka Kikosi cha awali cha Wachezaji 30 ni Leighton Baines, Michael Dawson, Tom Huddlestone, Scott Parker, Adam Johnson, Theo Walcott na Darren Bent.
Miongoni mwa Wachezaji hao 23 ni Kiungo wa Manchester City, Gareth Barry, ambae bado anauguza enka lakini amechukuliwa kwa mategemeo atapona.
Kikosi hicho kinaongozwa na Nahodha Rio Ferdinand.
England wapo Kundi C pamoja na USA, Algeria na Slovenia na watacheza mechi yao ya kwanza Juni 12 dhidi ya USA.
Kikosi kamili:
MAKIPA: Joe Hart, David James, Robert Green.
MABEKI: Jamie Carragher, Ashley Cole, Rio Ferdinand, Glen Johnson, Ledley King, John Terry, Matthew Upson, Stephen Warnock
VIUNGO: Gareth Barry, Michael Carrick, Joe Cole, Steven Gerrard, Frank Lampard, Aaron Lennon, James Milner, Shaun Wright-Phillips.
MAFOWADI: Peter Crouch, Jermain Defoe, Emile Heskey, Wayne Rooney
Wolves wamsaini Van Damme
Pengine Wadau watashtuka kuona Wolves imemsaini Van Damme lakini huyu si Yule Mcheza Sinema bali ni Beki wa Ubelgiki anaechezea Klabu ya Anderlecht aitwae Jelle Van Damme, miaka 26, na amesaini Mkataba wa Miaka mitatu kwa dau ambalo halikutangazwa.
Mwaka 2004/5, Van Damme alikuwa na Southampton na aliwahi kucheza mechi za Ligi Kuu.
Pia ameshawahi kuichezea Werder Bremen na ameichezea Timu ya Taifa ya Ubelgiji mechi 26.
Mtu 23 za Ivory Coast zatajwa!
Kocha wa Ivory Coast, Sven-Goran Eriksson, ametangaza majina ya Wachezaji 23 yatakayowasilishwa FIFA hapo kesho kwa ajili ya Fainali za Kombe la Dunia na Wachezaji maarufu waliobwagwa ni Bakary Kone na Kanga Akale.
Yale Majina mengine mazito ya kina Didier Drogba, Salamon Kalou, Aruna Dindane na Seydou Doumbia yapo kama ilivyotegemewa.
Ivory Coast wapo Kundi G pamoja na Brazil, Ureno na Korea Kaskazini.
Kikosi kamili:
MAKIPA: Boubacar Barry (Lokeren, Belgium), Aristides Zogbo (Maccabi Netanya, Israel), Daniel Yeboah (Asec, Ivory Coast).
MABEKI: Souleymane Bamba (Hibernian, Scotland), Arthur Boka (VB Stuttgart, Germany), Benjamin Brou Angoua (Valenciennes, France), Guy Demel (Hamburg SV, Germany), Emmanuel Eboue (Arsenal, England), Steve Gohouri (Wigan Athletic, England), Siaka Tiene (Valenciennes, France), Kolo Toure (Manchester City, England).
VIUNGO: Jean-Jacques Gosso Gosso(Monaco, France), Abdelkader Keita (Galatasaray, Turkey), Emmanuel Kone (International Curtea Arges, Romania), Gervinho (Lille, France), Koffi N'Dri Romaric (Sevilla, Spain), Cheik Ismael Tiote (Twente Enschede, Holland), Yaya Toure (Barcelona, Spain), Didier Zokora (Sevilla, Spain).
MAFOWADI: Aruna Dindane (Lekhwiya, Qatar), Didier Drogba (Chelsea, England), Salomon Kalou (Chelsea, England), Bakary Kone (Olympique Marseille, France).
McCarthy nje Afrika Kusini
Carlos Alberto Parreira hakumchukua Straika wa West Ham Benni McCarthy katika Timu yake ya Wachezaji 23 ya Afrika Kusini ambao ndio Wenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia litaloanza Juni 11.
Lakini Wachezaji wengine walio Ligi Kuu England, kama vile Steven Pienaar wa Everton na Mchezaji wa Fulham Kagiso Dikgacoi wamo.
Kikosi hicho kitaongozwa na Aaron Mokoena ambae ni Mlinzi wa Portsmouth.
McCarthy ndie Mchezaji anaeongoza kwa kufunga goli nyingi kwa Afrika Kusini na ana goli 31 katika mechi 79 alizochezea Timu ya Taifa na alikuwemo kwenye Vikosi vya Bafana Bafana vya Kombe la Dunia Mwaka 1998 na 2002.
Lakini tangu ajiunge na West Ham Februari 1 kutokea Blackburn Rovers amekuwa na maumivu ya goti na wengi wamekuwa wakimlaumu kwa kuongezeka uzito.
Afrika Kusini wapo Kundi A pamoja na Mexico, Uruguay na Ufaransa.
Kikosi kamili:
MAKIPA: Moeneeb Josephs (Orlando Pirates), Itumeleng Khune (Kaizer Chiefs), Shu-Aib Walters (Maritzburg United)
MABEKI: Matthew Booth, Siboniso Gaxa (both Mamelodi Sundowns), Bongani Khumalo (SuperSport United), Tsepo Masilela (Maccabi Haifa), Aaron Mokoena (Portsmouth), Anele Ngcongoa (Racing Genk), Siyabonga Sangweni (Lamontville Golden Arrows), Lucas Thwala (Orlando Pirates).
VIUNGO: Lance Davids (Ajax Cape Town), Kagisho Dikgacoi (Fulham), Thanduyise Khuboni (Lamontville Golden Arrows), Reneilwe Letsholonyane (Kaizer Chiefs), Teko Modise (Orlando Pirates), Surprise Moriri (Mamelodi Sundowns), Steven Pienaar (Everton), MacBeth Sibaya (Rubin Kazan), Siphiwe Tshabalala (Kaizer Chiefs).
MAFOWADI: Katlego Mphela (Mamelodi Sundowns), Siyabonga Nomvete (Moroka Swallows), Bernard Parker (FC Twente).
MATOKEO MECHI ZA KIRAFIKI ZA MATAIFA:
Jumatatu, 31 Mei 2010
Chile 3 Israel 0
Afrika Kusini 5 Guatemala 0
MECHI ZA LEO ZA KIRAFIKI:
Jumanne, 1 Juni 2010
Australia v Denmark, [saa 9 na nusu usiku]
Netherlands v Ghana, [saa 3 na nusu usiku]
Portugal v Cameroon, [saa 3 na nusu usiku]
Switzerland v Costa Rica, [saa 3 na robo usiku]

Monday 31 May 2010

Nigeria yataja 23 wa Bondeni!
Kocha wa Nigeria, Lars Lagerback, amewatupa nje Ikechukwu Uche wa Real Zaragoza na Straika wa Everton, Victor Anichebe, na kutangaza Kikosi chake cha mwisho cha Wachezaji 23 watakaokwenda Afrika Kusini katika Fainali za Kombe la Dunia zinazoanza Juni 11.
Katika Kikosi hicho yupo ‘majeruhi’ John Mikel Obi wa Chelsea ambae alikuwa akiuguza goti lake baada ya kufanyiwa operesheni.
Nigeria wapo Kundi B pamoja na Argentina, Ugiriki na Korea Kusini.
Mechi yao ya kwanza ni Juni 12 dhidi ya Argentina.
Kikosi kamili ni:
MAKIPA: Vincent Enyeama (Hapoel Tel Aviv, Israel), Dele Aiyenugba (Bnei Yehuda, Israel), Austin Ejide (Hapoel Petah Tikva, Israel)
MABEKI: Taye Taiwo (Marseille, France), Elderson Echiejile (Rennes, France), Chidi Odiah (CSKA Moscow, Russia), Joseph Yobo (Everton, England), Daniel Shittu (Bolton Wanderers, England), Ayodele Adeleye (Sparta Rotterdam, Netherlands), Rabiu Afolabi (SV Salzburg, Austria)
VIUNGO: Chinedu Ogbuke Obasi (TSG Hoffenheim, Germany), John Utaka (Portsmouth, England), Kalu Uche (Almeria, Spain), Dickson Etuhu (Fulham, England), John Mikel Obi (Chelsea, England), Sani Kaita (Alaniya, Russia), Haruna Lukman (AS Monaco, France), Yusuf Ayila (Dynamo Kiev, Ukraine), Osaze Odemwingie (Lokomotiv Moscow, Russia)
MASTRAIKA: Yakubu Aiyegbeni (Everton, England), Nwankwo Kanu (Portsmouth, England), Obafemi Martins (Wolfsburg, Germany), Victor Obinna Nsofor (Malaga, Spain)
Mourinho atua Real na kutamba: “Mimi ni Jose Mourinho na sibadiliki! Nimetua na vipaji vyangu na kasoro zangu!”
Leo Jose Mourinho ametangazwa rasmi kama Meneja mpya wa Real Madrid kuchuku nafasi ya Manuel Pellegrini kutoka Chile na amesaini Mkataba wa Miaka minne.
Mourinho, mwenye Miaka 47, anakuwa Meneja wa 11 wa Real katika kipindi cha Miaka 7 iliyopita.
Real Madrid haijatwaa Kombe lolote kwa Miaka miwili sasa na uteuzi wa Mourinho ambae wiki moja iliyopita alitwaa Kombe la Klabu Bingwa akiwa na Inter Milan ni hatua ya kurekebisha kasoro hiyo kwa Timu iliyotumia zaidi ya Pauni Milioni 200 kuwanunua Masupastaa Ronaldo, Kaka, Alonso na Benzema hapo Mwaka jana.
HISTORIA YA MOURINHO KAMA MENEJA
-Benfica (2000)
-Uniao de Leiria (2000-02)
-Porto (2002-04) –Ubingwa wa Ligi mara 2, Kombe la Ureno, UEFA Cup mara 1, UEFA CHAMPIONS LEAGUE mara 1.
-Chelsea (2004-07) –Ubingwa wa Ligi Kuu mara 2, Carling Cup mara 2, FA Cup mara 1.
-Inter Milan (2008-10) -Ubingwa Serie A mara 2, Coppa Italia mara 1, UEFA CHAMPIONS LEAGUE mara 1.
Everton yamsaini Beckford
Everton imemsaji Straika hatari Jermaine Beckford kwa Mkataba wa Miaka minne na Mchezaji huyo kutoka Leeds United amesajiliwa kama Mchezaji huru kwa vile Mkataba wake na Leeds umemalizika.
Beckford ndie alieiwezesha Leeds kupanda Daraja na Msimu ujao itacheza Daraja la Coca Cola Championship ambalo liko chini tu ya Ligi Kuu.
Mchezaji huyo mwenye miaka 26 aliifungia Leeds mabao 31 Msimu uliopita na moja ya hayo ni lile bao lililowang’oa Manchester United kwa bao 1-0 kwenye Raundi ya 3 ya FA Cup Uwanjani Old Trafford Mwezi Januari.
MATOKEO MECHI ZA KIRAFIKI ZA MATAIFA:
Jumapili, 30 Mei 2010
Belarus 1 v South Korea 0
Japan 1 v England 2
Mexico 5 v Gambia 1
Nigeria 1 v Colombia 1
Paraguay 2 v Ivory Coast 2
Tunisia 1 v France 1

Sunday 30 May 2010

England 2 Japan 1, Goli zote wafunga Japan!!!
Magoli mawili ya kujifunga wenyewe leo yamewapa ushindi England wa bao 2-1 dhidi ya Japan huko Graz, Austria katika mechi ambayo Kocha wa England aliwaacha benchi Mastaa kadhaa na kimchezo England walipwaya mno.
Japan walipata bao lao dakika ya 6 baada ya Beki Marcus Tulio Tanaka kuwasha bunduki baada ya kona ya Yasuhito Endo na mpira kumpita Kipa David James.
Hadi mapumziko Japan walikuwa mbele kwa bao 1-0.
Kipindi cha pili, dakika ya 56, Frank Lampard alishindwa kufunga penalti iliyookolewa na Kipa Eiji Kawashima.
England walipewa penalti hiyo Endo alipounawa mpira kufuatia frikiki ya Lampard.
Kipindi hicho cha Pili, Capello aliwatoa Wachezaji watano kina David James, Johnson, Huddlestone, Walcott na Bent na kuwaingiza Joe Hart, Jamie Carragher, Joe Cole, Shaun Wright-Phillips na Steven Gerrard.
Mabadiliko hayo yalileta uhai kwa England na presha yao ilizawadiwa kwa Japan kujifunga wenyewe bao mbili.
Bao la kwanza lilifungwa dakika ya 72 kufuatia krosi ya Joe Cole kupigwa kichwa na beki wa Japan Marcus Tulio Tanaka na kutinga wavuni.
Bao la pili pia lilitokana na krosi, na safari hii ilikuwa krosi ya Ashley Cole, iliyofungwa na Beki wa Japan Nakazawa.
Vikosi vilikuwa:
England: David James (Joe Hart, 46), Glen Johnson (Jamie Carragher, 46), Ashley Cole, Tom Huddlestone (Steven Gerrard, 46), Rio Ferdinand, John Terry, Theo Walcott (Shaun Wright-Phillips, 46), Frank Lampard, Darren Bent (Joe Cole, 46), Wayne Rooney, Aaron Lennon (Emile Heskey, 77).
Japan: Eiji Kawashima, Yuji Nakazawa, Marcus Tanaka, Yuto Nagatomo, Yusuyuki Konno, Yasuhito Endo (Keiji Tamada, 86), Makoto Hasebe, Abe Yujki, Keisuke Honda, Yoshito Okubu (Daisuke Matsui, 72), Shinji Okazaki (Takayuki Morimoto, 65).
MATOKEO MECHI ZA KIRAFIKI ZA MATAIFA:
Jumamosi, 29 Mei 2010
Azerbaijan 1 v FYR Macedonia 3
Hungary 0 v Germany 3
Iceland 4 v Andorra 0
New Zealand 1 v Serbia 0
Norway 2 v Montenegro 1
Poland 0 v Finland 0
Slovakia 1 v Cameroon 1
Spain 3 v Saudi Arabia 2
Sweden 4 v Bosnia-Hercegovina 2
Ukraine 3 v Romania 2
United Arab Emirates 3 v Moldova 2
USA 2 v Turkey 1
MECHI ZA KIMATAIFA ZA KIRAFIKI
[saa za kibongo]
Jumapili, 30 Mei 2010
Belarus v South Korea, [saa 10 jioni]
Chile v Northern Ireland, [saa 5 usiku]
Japan v England, [saa 9 na robo mchana]
Mexico v Gambia, [saa 12 jioni]
Nigeria OFF Colombia, [saa 3 usiku]
Paraguay v Ivory Coast, [saa 3 usiku]
Tunisia v France, [saa 3 usiku]
Venezuela v Canada, [saa 8 na nusu usiku]
Powered By Blogger