Saturday 25 October 2008

West Brom 0 Hull City 3

Hull City imeendeleza wimbi la kuwashangaza wengi kwa kushinda mechi tena ugenini na sasa kuwa nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi nyuma ya Chelsea na Liverpool na juu ya Arsenal na Man U.
Mabao matatu yalifungwa na Zayatte dakika ya 47, Geovanni dakika ya 62 na King ya 66.

Blackburn 1 Middlesbrough 1

Benny McCarthy, Mchezaji kutoka Afrika Kusini alieingizwa kipindi cha pili, ameiokoa timu yake Blackburn baada ya kusawazisha dakika za majeruhi kwa kichwa safi.

Afonso Alves aliipa Middlesbrough bao la kuongoza kwenye dakika ya 74.
Sunderland 2 Newcastle 1

Frikiki tamu aliyopiga Kieron Richardson dakika ya 75 imewapa Sunderland ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Newcastle kweenye mechi ya ligi iliyochezwa nyumbani kwa Sunderland uwanja wa Stadium of Light.
Djibril Cisse aliipatia Sunderland bao la kwanza lakini Shola Ameobi akasawazisha kwa kichwa.

Sunderland: Fulop, Chimbonda, Ferdinand, Collins, McCartney, Malbranque, Whitehead, Yorke, Richardson, Cisse, Diouf.
Akiba: Colgan, Bardsley, Tainio, Chopra, Jones, Leadbitter, Reid.
Newcastle: Given, Beye, Taylor, Coloccini, Bassong, Geremi, Guthrie, Butt, Duff, Ameobi, Martins.
Akiba: Harper, Jose Enrique, Cacapa, Barton, N'Zogbia, Gutierrez, Xisco.
Mabingwa Man U wavutwa shati!: Everton 1 Man U 1

Mabingwa wa LIGI KUU, Man U, baada ya kutawala kipindi cha kwanza na kuongoza kwa bao la Darren Fletcher, walilazimishwa sare ya 1-1 na Everton kwenye mechi ya ligi iliyochezwa Goodison Park.
Everton walisawazi kipindi cha pili kwa bao lililofungwa na Fellaini.
Hii ni mechi ambayo Man U wataona ni kama wametupa pointi 2 kwani walikuwa na kila nafasi ya kupata bao la 2.
Wenger amuwakia Nahodha wake Gallas kwa kupigwa picha naiti klabu usiku wa manane!!!

Meneja wa Arsenal Arsene Wenger amewaka na kudai picha aliyopigwa Gallas akitoka ndani ya naiti klabu huko London usiku wa manane huku ana sigara mdomoni haikubaliki kwa maadili ya klabu na atazungumza na kumpa onyo kali Nahodha wake.
'Nitazungumza nae!' Wenger amesesema. 'Ni lazima ajue wajibu wake kama Nahodha wa klabu!'
William Gallas ambae hajacheza mechi hivi karibuni baada ya kuumia paja amepona na anategemewa kucheza mechi na West Ham Jumapili.
Msimu uliopita Gallas alipondwa sana kwa kuonyesha tabia asiyostahili kwa Nahodha pale alipoamua kukaa chini katikati ya uwanja kwenye mechi waliyotoka sare na Birmingham wakati mpira unaendlea na wakati huo inasemekana Wenger alitaka kumnyang'anya Unahodha.

Real Madrid wabwaga manyanga kwa Ronaldo!

Rais wa Real Madrid Ramon Calderon amesema klabu yake haina haja tena ya kumnunua Cristiano Ronaldo kwani Manchester United hawataki kumuuza.
Ronaldo ana mkataba na Mabingwa wa Uingereza na Ulaya Manchester United unaoisha mwaka 2010.
Real Madrid walijaribu kumrubuni sana Ronaldo kabla msimu haujaanza na ilibidi Man U wawashitaki Real kwa FIFA.
Calderon amedai: 'Manchester United ni klabu kubwa duniani na hatutaki mzozo nao na wakisema hawauzi mtu basi huwezi kufanya kitu ni bora uliache hilo suala.'
Nae Sir Alex Ferguson ametamka waziwazi Owen Hargreaves hauzwi baada ya kuibuka minong'ono kwamba mchezaji huyo ni majeruhi muda mwingi basi ni bora auzwe.
Ferguson ametamka: 'Kwa ajili ya Hargreaves bora nitamke waziwazi hauzwi na wala hatujafikiria hilo!'
'Kwa sasa yuko kwenye matibabu na anendelea vizuri.' Ferguson aliongeza. 'Haya magazeti kutangaza anauzwa ni stori nzuri kwao kwa sababu tu kacheza mechi 2 tu msimu huu! Wanasahau msimu uliopita alitusaidia sana kushinda LIGI KUU na Ubingwa wa Ulaya!'
Tangu Hargreaves atue Man U akitokea Bayern Munich kwa dau la Pauni Milioni 18 ameandamwa na tatizo la goti linalopona na kurudi tena na amekosa mechi nyingi.

Friday 24 October 2008

RATIBA YA LIGI KUU UINGEREZA

Baada ya michuano ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE na UEFA CUP iliyofanyika katikati ya wiki sasa macho yetu yako wikiendi hii kwenye kitimtim cha LIGI KUU na safari hii timu zote zitacheza mechi wikiendi na vilevile kuwa na mechi nyingine kati ya wiki siku ya Jumatano isipokuwa Newcastle na West Brom watakao kutana siku ya Jumanne.
Bila shaka macho ya wengi yatakuwa kwenye mechi ya Jumapili ya Chelsea v Liverpool timu ambazo ndio zinaongoza LIGI KUU kwa sasa na ambazo hazijafungwa.

Jumamosi, 25 Oktoba 2008

Everton v Man U [saa 8 mchana]

Sunderland v Newcastle [saa 8 dakika 45 mchana]

West Brom v Hull City [saa 11 jioni]

Blackburn v Middlesbrough [saa 1 na nusu usiku]

Jumapili, 26 Oktoba 2008

Chelsea v Liverpool [saa 9 na nusu mchana]

Man City v Stoke City [saa 11 jioni]

Tottenham v Bolton [saa 11 jioni]

Wigan v Aston Villa [saa 11 jioni]

Portsmouth v Fulham [saa 1 usiku]

Jumanne, 28 Oktoba 2008

Newcastle v West Brom [saa 4 dakika 45 usiku]

Jumatano, 29 Oktoba 2008

[saa 4 dakika 45 usiku]

Aston Villa v Blackburn

Hull City v Chelsea

Stoke City v Sunderland

[saa 5 usiku]

Arsenal v Tottenham

Bolton v Everton

Fulham v Wigan

Liverpool v Portsmouth

Man U v West Ham

Middlesbrough v Man City
UEFA CUP: Portsmouth wafa Ureno, Aston Villa washinda Uingereza!!

Baada ya kipigo cha Tottenham cha mabao 2-0 walichopewa na Udinese huko Italia, Portsmouth nao wameuawa huko Ureno na Klabu ya Braga iliyowabandika bao 3-0 wakati Aston Villa wakiwa nyumbani Uingereza wamejikongoja kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Ajax ya Uholanzi.
Portsmouth walijikuta wako nyuma bao moja pale frikiki ya Luis Aguiar ya umbali wa mita 30 kumhadaa Kipa David James na kutikisa nyavu.
Sekunde 90 tangu kipindi cha pili kuanza Wason Renteria wa Braga akapachika la pili na dakika chache kabla mechi kwisha Osorio Alan akaweka bao la 3.

Nao Aston Villa wakiwa uwanjani kwao Villa Park walianza mechi wakielemewa na Ajax lakini Nahodha Martin Laursen alifunga kwa kichwa cha nguvu kufuatia kona iliyochongwa na Ashley Young dakika ya 8.
Ajax waliendelea kutawala mechi na haikushangaza pale waliposawazisha kwenye dakika ya 22 kufuatia kona ya Urby Emanuelson kufungwa kwa kichwa na Thomas Vermaelen.
Lakini Aston Villa walipachika bao la pili na la ushindi dakika ya 45 baada ya kazi nzuri ya Ashley Young kumaliziwa vizuri na Gareth Barry.
MATOKEO YA MECHI NYINGINE ZA UEFA CUP ZA LEO:
AS Nancy 3 Feyenoord 0
CSKA Moscow 3 Deportivo la Coruna 0
Dinamo Zagreb 3 NEC 2
FC Copenhagen 1 St Etienne 3
Twente Enschede 1 Racing Santander 0
Galatasaray 1 Olympiacos 0
Heerenveen 1 AC Milan 3
Hertha Berlin 1 Benfica 1
MSK Zilina 1 Hamburg 2
Partizan Belgrade 1 Sampdoria 2
Schalke 04 3 PSG 1
Sevilla 2 Vfb Stuttgart 0
Rosenborg 0 Club Bruges 0
FA YAIFUTA KADI NYEKUNDU YA BEYE WA NEWCASTLE

Kamati ya Sheria ya FA leo imeifuta kadi nyekundu aliyopewa Beki wa Newcastle Habib Beye kwenye dakika 13 tu ya mchezo na Manchester City na Refa Rob Styles ambae pia alitoa penalti iliyofungwa na Robinho.
Katika mechi hiyo, Newcastle waliocheza watu 10 tangu dakika hiyo ya 13 walitoka suluhu ya 2-2 na Manchester City.
Hii inamaanisha adhabu ya kufungiwa ya kutocheza mechi moja ya Mchezaji huyo raia wa Senegal nayo pia imeondolewa.
Marudio ya video yalidhihirisha Habib Beye alicheza mpira na hakumchezea faulo Robinho [pichani].
Hii ina maana Beye yuko huru kucheza mechi ya Jumamosi wakati Newcastle watakapopambana na Sunderland.

Thursday 23 October 2008

UEFA CUP: Udinese 2 Tottenham 0

Tottenham, klabu ambayo iko mkiani LIGI KUU UINGEREZA, leo tena imebamizwa mabao 2-0 na Timu ya Italia, Udinese, kwenye mechi ya kugombea Kombe la UEFA.
Msimu wa Tottenham unaonyesha sasa klabu ipo majaribuni na sasa hata Wachezaji wameanza kunung'unika waziwazi kama alivyofanya Mchezaji David Bentley alielalamikia mwanzo mbovu wa Tottenham msimu huu hali iliyomfanya Meneja Juande Ramos amtoe kwenye kikosi cha leo.
Uwanjani mambo yaliendelea kwenda mrama pale Kipa wao Heurelho Gomes katika dakika ya 24 aliposhindwa kumiliki pasi aliyorudishiwa na Beki wake na katika kupapatika akamchezea rafu Fabio Quagliarella wa Udinese, Refa akatoa penalti iliyofungwa na Antonio Di Natale.
Balaa haikushia hapo.
Kiungo wao John O'Hara akachezea rafu mbili ndani ya dakika moja na kila rafu aliyocheza akazawadiwa kadi ya njano hivyo akatwangwa nyekundu na akatolewa nje ya uwanja.
Msumari wa mwisho kwa Tottenham uligongomezwa dakika ya 86 ya mchezo pale Pepe alipoifungia Udinese bao la pili.

UEFA CUP: Timu za LIGI KUU zajimwaga uwanjani!

Leo timu kadhaa za Ulaya zinajitupa uwanjani katika kuwania UEFA CUP ikiwa pamoja na timu za Uingereza Aston Villa, Portsmouth na Tottenham.
Timu hizi zimegawanywa katika Makundi mbalimbali na zinacheza ule mtindo wa nyumbani na ugenini.

Baadhi ya mechi zitakazochezwa leo ni:


Aston Villa v Ajax

Braga v Portsmouth

Udinese v Tottenham

CSKA Moscow v Deportivo La Coruna,

Dinamo Zagreb v NEC,

FC Copenhagen v St Etienne,

FC Twente v Racing Santander,

Galatasaray v Olympiacos,

Heerenveen v AC Milan,

Hertha Berlin v Benfica,

MSK Zilina v Hamburg,

Partizan Belgrade v Sampdoria,

Rosenborg v Club Brugge,

Schalke 04 v PSG,

Sevilla v VfB Stuttgart,
Liverpool suluhu, Chelsea ushindi kiduchu!!

Jana kwenye UEFA CHAMPIONS LEAGUE, Liverpool wakicheza ugenini huko Madrid, Spain waliambulia sare ya ba0 1-1 na Atletico Madrid.
Robbie Keane aliwapatia Liverpool bao lao kwenye dakika ya 14 na Simao akaisawazishia Atletico Madrid dakika ya 83.
Atletico Madrid: Franco, Seitaridis, Perea, Dominguez, Antonio Lopez, Camacho (Raul Garcia 72), Maniche, Luis Garcia (Aguero 46), Simao, Forlan, Sinama Pongolle (Miguel 75).
AKIBA [hawakucheza]: Bernabe, Pernia, Heitinga, Paulo Assuncao.
KADI: Maniche.
Liverpool: Reina, Arbeloa, Carragher, Agger, Dossena, Mascherano, Alonso (Leiva Lucas 75), Benayoun, Gerrard (Babel 61), Riera, Keane (Kuyt 53).
AKIBA [hawakucheza]: Cavalieri, Aurelio, Pennant, Darby.
KADIRiera, Arbeloa.
WATAZAMAJI: 44,500
REFA: Claus Bo Larsen (Denmark).

Goli lililofungwa na Nahodha John Terry kwa kichwa kufuatia kona ya Frank Lampard dakika ya 78 liliwapa ushindi wa bao 1-0 Chelsea waliokuwa uwanja wao Stamford Bridge dhidi ya AS Roma ya Italy.
Ilikuwa ni mechi iliyopooza huku Chelsea wakicheza bila ushirikiano na AS Roma wakijaza wachezaji wengi kwenye kiungo.
Chelsea: Cech, Bosingwa, Terry, Carvalho, Bridge, Kalou (Di Santo 77), Lampard, Mikel, Malouda (Belletti 46), Deco, Anelka (Ferreira 90).
AKIBA [hawakucheza]: Cudicini, Ivanovic, Alex, Stoch.
KADI: Malouda, Terry.
Roma: Doni, Cicinho, Panucci, Mexes, Riise (Tonetto 82), De Rossi, Brighi, Aquilani (Perrotta 60), Taddei (Menez 81), Totti, Vucinic.
AKIBA [hawakucheza]: Artur, Loria, Montella, Okaka Chuka.
KADI: Mexes, Panucci.
WATAZAMAJI: 41,002
REFA: Kyros Vassaras (Greece).

MATOKEO MECHI NYINGINE ZA UEFA CHAMPIONS LEAGUE:

Basle 0 Barcelona 5

Bordeaux 1 CFR Cluj-Napoca 0

Inter Milan 1 Anorthosis Famagusta 0

PSV Eindhoven 2 Marseille 0

Panathanaikos 2 Werder Bremen 2

Shakhtar Donetsk 0 Sporting Lisbon 1

Wednesday 22 October 2008

BUNDUKI ZETU NDOGO HAZINA WOGA-Wenger adai!!!

Meneja wa Arsenal Arsene Wenger amekisifia kikosi chake chenye chipukizi wengi kilichowabamizi Fenerbahce jana kwenye pambano la UEFA CHAMPIONS LEAGUE kwa mabao 5-2.
Arsenal, wakicheza ugenini nchini Uturuki, walikuwa na Wachezaji wenye wastani wa umri wa miaka 22 uwanjani na vilevile walimuingiza Mchezaji mdogo kutoka Wales Aaron Ramsey mwenye miaka 17 na akamudu kupachika bao la 5.
Wenger alikipamba kikosi chake kwa kudai: 'Timu yetu ni changa lakini nasikia furaha kwa kuona tumeweza kuja hapa ugenini na kutawala mchezo! Kasi yetu, kuzunguka kwetu uwanjani na utalaam wetu ndio silaha yetu iliyotufanya tuimiliki gemu!'

Berbatov amchengua Ferguson!

Bosi wa Manchester United Sir Alex Ferguson amefurahishwa na uchezaji wa Mshambuliaji wake Dimitar Berbatov baada ya kufunga mabao mawili kati ya matatu katika ushindi dhidi ya Celtic hapo jana kwenye mechi ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE.
Sir Alex Ferguson alitamka: 'Ni kazi nzuri sana amefanya! Sasa anatuletea ustadi na utulivu kwenye mashambulizi! Bila shaka ushirikiano wake na Rooney na Tevez utaboreka zaidi!'
Berbatov alishindwa kufunga goli katika mechi zake nne za kwanza alizochezea Man U lakini sasa ameshafunga magoli matano katika mechi nne.

DRO YA NCHI ZA AFRIKA KUELEKEA FAINALI KOMBE LA DUNIA 2010 YAFANYIKA MJINI ZURICH, USWISI

Nchi za Afrika 20 zilizofuzu kuingia hatua ya mwisho kutafuta wawakilishi wa Bara la Afrika katika FAINALI ZA KOMBE LA DUNIA 2010 zitakazofanyika huko Afrika Kusini leo zimegawanywa katika Makundi matano ya Nchi 4 kila moja ambapo mshindi wa kila Kundi ndie atakaeingia FAINALI ZA KOMBE LA DUNIA 2010 kujumuika na Mwenyeji wa mashindano Afrika Kusini.
Washindi watatu wa kwanza wa kila Kundi wataingia FAINALI ZA KOMBE LA MATAIFA YA AFRIKA zitakazofanyika huko Angola pia mwaka 2010.

Mgawanyo wa MAKUNDI ni:

KUNDI A: Cameroun, Morocco, Gabon, Togo

KUNDI B: Nigeria, Tunisia, Kenya, Mozambique

KUNDI C: Egypt, Algeria, Zambia, Rwanda

KUNDI D: Ghana, Mali, Benin, Sudan

KUNDI E: Ivory Coast, Guinea, Burkina Faso, Malawi
Baada ya Man U na Arsenal kung'ara jana, leo Chelsea na Liverpool vitani!!

Jana Mabingwa watetezi Man U na Arsenal walifuzu kuzipa sifa Klabu za Uingereza sasa leo usiku ni zamu ya Chelsea ambao watakuwa kwao Stamford Bridge wakipambana na AS Roma ya Italy na Liverpool watakuwa wageni wa Atletico Madrid kwenye Uwanja wa Vicente Calderon.

ATLETICO MADRID v LIVERPOOL

Liverpool leo watashuka uwanjani bila ya Mfungaji wao bora Fernando Torres pamoja na Beki wa kati Martin Skrtel kwani wote ni majeruhi.
Kipa wa Liverpool Jose Reina, ambae baba yake mzazi alichezea Atletico Madrid, amewaonya Wachezaji wenzake kuhusu Atletico Madrid kwa kutamka: 'Wana mastaa hatari sana kama Diego Forlan, Sergio Aguero na Florent Sinama-Pongolle.'
Timu ya Liverpool inategemewa kuchaguliwa kutoka: Reina, Arbeloa, Carragher, Agger, Dossena, Pennant, Gerrard, Alonso, Riera, Keane, Kuyt, Lucas, Insua, Ngog, Benayoun, El Zhar, Mascherano, Cavalieri.

CHELSEA V AS ROMA

Majeruhi wa Chelsea ambao hawajacheza mechi kadhaa za hivi karibuni huenda leo wakapata namba na hao ni Deco, Joe Cole na Kipa Petr Cech.
Nao AS Roma wanategemewa kuwarudisha tena kikosini Philippe Mexes na Christian Panucci waliokuwa na kifungo cha mechi za huko Italia pamoja na Nahodha Francesco Totti aliefanyiwa opersheni ya goti ambae alianza kucheza mechi yake ya kwanza siku ya Jumapili walipofungwa 4-0 na Inter Milan.
Wachezaji watakaowakilisha Chelsea wanategemewa kuwa: Cech, Hilario, Cudicini, Ivanovic, Ferreira, Malouda, Obi, Deco, Kalou, Bosingwa, Terry, Lampard, Anelka, Belletti, Alex, Carvalho, Mancienne, Bridge, Di Santo, J Cole.

MECHI ZA LEO JUMATANO, 22 October 2008


[Saa 3 dak 45 usiku]

Atletico Madrid v Liverpool,

Basle v Barcelona,

Bordeaux v CFR Cluj-Napoca,

Chelsea v Roma,

Inter Milan v Anorthosis Famagusta,

Panathinaikos v Werder Bremen,

PSV v Marseille,

Shakhtar Donetsk v Sporting,
BECKHAM AJIUNGA AC MILAN KWA MKOPO

Nyota wa Uingereza David Beckham, miaka 33, atajiunga na Klabu ya Italia AC Milan kwa mkopo kuanzia Januari mwakani hadi mwisho wa msimu huu.
Kwa sasa Beckham ni Mchezaji wa Klabu ya Los Angeles Galaxy ya Marekani ambao msimu wao wa ligi unakwisha wikiendi hii na kuanza msimu mpya ni mpaka Aprili mwakani na hii inamaanisha Beckham angekuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu hivyo kuhatarisha hata uteuzi wake kwenye Timu ya Taifa ya Uingereza.
Beckham anahitaji achezee Timu ya Taifa ya Uingereza mechi mbili tu zaidi ili avunje rekodi ya Bobby Moore aliyochezea mechi 108 ingawa rekodi ya mechi nyingi inashikiliwa na Kipa Peter Shilton aliecheza mechi 128.
Akiwa AC Milan atajiunga na mastaa wa Brazil kama Ronaldinho, Kaka na Alexandre Pato pamoja na wa Italy kama Andrea Pirlo na Gennaro Gattuso.
MAN U NA ARSENAL ZAPETA UEFA CHAMPIONS LEAGUE!!!!

Timu za Uingereza Manchester United ambao ndio Mabingwa Watetezi wa UEFA CHAMPIONS LEAGUE na Arsenal jana zilipata ushindi murua katika mechi zao wakati Man U walipowabandika wapwa zao Celtic mabao 3-0 uwanjani kwake Old Trafford huku Arsenal akishinda ugenini Uturuki alipoichabanga Fenerbahce mabao 5-2.
Mabao ya Man U yaligungwa na Dimitar Berbatov mabao mawili na Wayne Rooney bao 1.
Wafungaji wa Arsenal walikuwa ni Adebayor, Walcott, Diaby, Song Billong na Ramsey.

Matokeo mengine ya mechi hizo za UEFA CHAMPIONS LEAGUE ni kama ifuatavyo:

Bayern Munich 3 Fiorentina 0

FC Porto 0 Dynamo Kiev 1

Juventus 2 Real Madrid 1

Steau Buchares 3 Lyon 5

Villareal 6 Aalborg 3

Zenit St Petrsburg 1 BATE Borisov 1

Tuesday 21 October 2008

MAN U na ARSENAL wanashuka dimbani leo kwenye UEFA CHAMPIONS LEAGUE

Leo, katika michuano ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE, Mabingwa wa Kombe hilo, Mancheter United, wanawakaribisha Old Trafford wajomba zao Celtic ambao ni Mabingwa wa Scotland katika mechi iliyobatizwa 'Mapigano ya Uingereza'.
Huko Uturuki, Arsenal watakuwa wageni wa Fenerbahce katika mechi itakayokuwa ya vuta ni kuvute kwani daima timu za Kituruki huvimba sana wakiwa nyumbani kwao.
Katika mechi iliyopita, Manchester United waliwafunga Aalborg ya Denmark hukohuko Denmark kwa mabao 3-0 wakati Arsenal walipata ushindi uwanjani kwake Emirates walipoibandika FC Porto ya Ureno mabao 4-0.
Kikosi cha Arsenal leo kitashuka bila ya Kolo Toure, William Gallas na Bacary Sagna ambao wote ni majeruhi.
Kikosi cha Arsenal kinatazamiwa kuwa: Almunia, Song, Silvestre, Clichy, Eboue, Fabregas, Denilson, Nasri, Diaby, Walcott, Van Persie, Adebayor, Fabianski, Vela, Ramsey, Gibbs, Hoyte, Bendtner, Djourou.
Nao Manchester United watawakosa Paul Scholes, Owen Hargreaves, Michael Carrick na Patrice Evra kwani wote ni majeruhi.
Meneja wa Man U Sir Alex Ferguson amedokeza pia huenda akampumzisha Ronaldo na kumchezesha Nani badala yake ingawa hakuthibitisha kwa hilo.
Kikosi cha Man U kitatokana na: Van der Sar, Kuszczak, Brown, Neville, Rafael, Ferdinand, Vidic, Evans, O'Shea, Ronaldo, Nani, Fletcher, Anderson, Giggs, Gibson, Park, Tevez, Berbatov, Rooney, Manucho.
Nao Celtic watashusha kikosi kutoka kwa: Boruc, Caldwell, Wilson, McManus, Loovens, Naylor, McGeady, S Brown, Hinkel, Hartley, Robson, McDonald, Sheridan, Maloney, M Brown, McCourt, Hutchinson, Nakamura, O'Dea.
REFA ALIETOA PENALTI TATA KWA MAN CITY AKUBALI KUIANGALIA UPYA NA KUTOA UAMUZI WAKE!!

Refa Rob Styles, aliewapa Manchester City penalti tata dakika ya 13 tu ya mchezo na vilevile kumlima Beki wa Newcastle Habib Beye kadi nyekundu kwa tukio hilo ambalo marudio ya video yamedhihirisha Habib Beye alicheza mpira na hakumchezea faulo Robinho [pichani], amekubali kulitazama upya tukio hilo na kutoa uamuzi kama ni sahihi au alikosea.
Hatua hii ya Refa Rob Styles kupitia upya uamuzi wake imethibitishwa na Meneja wa Newcastle Joe Kinnear ambae amesema: 'Niliongea na Rob Styles na amekubali kuliangalia upya na kama akiona amekosea basi kadi nyekundu kwa Beye itafutwa. Sisi tunamshkuru kwani sote ni binadamu na huwa tunakosea. Kukubali umekosea ni ushujaa wa hali ya juu!'
Katika mechi hiyo ya jana licha ya kucheza Wachezaji 10 tangu dakika ya 13 na kufungwa bao hilo la penalti, Newcastle walikuwa wanaongoza hadi dakika ya 85 ndipo Man City wakasawazisha na mechi kuisha kwa mabao 2-2.
Nao FA wamethibitisha Kamati yao ya Nidhamu itapitia tukio hilo la Beye kulimwa kadi nyekundu na kuamua kuifuta au kuiacha hiyo kadi siku ya Alhamisi.
UEFA CHAMPIONS LEAGUE: JUMANNE, 21 October 2008

[Saa 3 dak 45 usiku]

Bayern Munich v Fiorentina,

FC Porto v Dynamo Kiev,

Fenerbahce v Arsenal,

Juventus v Real Madrid,

Man United v Celtic,

Steaua Bucuresti v Lyon,

Villarreal v AaB,

Zenit St Petersburg v BATE, [Saa 2 na nusu usiku]
Newcastle 2 Manchester City 2

Manchester City ilijiokoa kutoka kipigo dhidi ya Timu iliyocheza na watu 10 tu kwa muda mrefu wa mchezo baada ya Beki wa Newcastle Habib Beye kutolewa nje kwa kadi nyekundu kwenye dakika ya 13 tu ya mchezo baada ya Refa Rob Styles kudhani amemchezea rafu Robinho na pia kutoa penalti iliyofungwa na Robinho.
Tukio hilo liliwaudhi sana Newcastle kwani ilikuwa dhahiri sio penalti.
Shola Ameobi aliisawazishia Newcastle dakika ya 44.
Kipindi cha pili Beki wa Man City Richard Dunne alijifunga mwenyewe na kuwafanya Newcastle waongoze 2-1 hadi dakika ya 85 wakati Stephen Ireland aliposawazisha.
Newcastle: Given, Beye, Taylor, Coloccini, Bassong, Geremi, Guthrie, Butt, Duff, Martins (N'Zogbia 72), Ameobi (Carroll 79).AKIBA: Harper, Cacapa, Jose Enrique, Xisco, Edgar.
Man City: Hart, Richards (Onuoha 58), Ben-Haim, Dunne, Garrido (Sturridge 83), Wright-Phillips, Kompany, Hamann (Evans 64), Ireland, Jo, Robinho.AKIBA: Schmeichel, Elano, Fernandes, Berti.
WATAZAMAJI: 45,908

Monday 20 October 2008

FERGUSON AMWOKOA MTANGAZAJI!

Mtangazaji wa Michezo wa Kituo cha TV maarufu huko Uingereza ITV, Jim Rosenthal, ambae aliondolewa kazini bila kutarajia ameokolewa na Meneja wa Manchester United Sir Alex Ferguson na sasa amerudishwa tena kibaruani.
Jim Rosenthal, mwenye umri wa miaka 60, ambae ameitumikia ITV kwa miaka 28, aliambiwa mwezi Januari mwaka huu kuwa mkataba wake ukiisha haongezewi tena!
Alionekana kwenye luninga kwa mara ya mwisho mwezi Juni mwaka huu.
Hivi karibuni, Sir Alex Ferguson, akiwa mgeni mwalikwa kwenye hafla ya hisani, alitoa ombi maalum kwa wageni wenzake waalikwa ambao wengi walikuwa ni nyota mbalimbali kwenye michezo na watu maarufu: 'Jim Rosenthal alikuwa Mtangazaji bora wa TV. Sasa hana kazi. Naomba kila mtu awaandikie ITV na kuwataka arudishwe kazini. Ni Mtangazaji bora sana lakini Mabosi wake wanasema ni mzee!'
Sasa Jim Rosenthal amepewa mkataba mpya wa miaka minne na atasimamia mechi za Kombe la FA na Masumbwi.
Mwenyewe Jim Rosenthal anasema: 'Ni kweli Sir Alex Ferguson amenisaidia sana! Nilipata mstuko mkubwa nilipoambiwa sina kazi tena! Utangazaji ni maisha yangu! Ferguson anasaidia watu wengi sana lakini hataki ajulikane kwa hilo! Alipotamka maneno yale mazuri kuhusu mimi kwenye ile hafla ilinigusa sana na vitu kama hivi mabosi wanasikiliza! Nilikuwa na wakati mgumu lakini huo ndio wakati unaogundua nani rafiki wako wa kweli!'
Na, bila shaka, Sir Alex Ferguson ni rafiki yake bora na wa kweli kikweli!

Sunday 19 October 2008

'NYODO' DROGBA:
=Ateuliwa tena kuwa miongoni mwa wagombea MCHEZAJI BORA AFRIKA 2008 licha ya kususia mwaka 2007!

=Adai angempiga ngumi Nemanja Vidic wa Man U!

Didier Drogba wa Chelsea na Nchi ya Ivory Coast ameteuliwa kuwa miongoni mwa wagombea wa Tuzo ya Mchezaji Bora wa Afrika 2008 licha ya kususia sherehe za kukabidhi Tuzo hiyo mwaka jana huko nchini Togo ambako alitegemewa kushinda Tuzo hiyo kwa mara ya pili mfululizo baada ya kuitwaa ile ya mwaka 2006.
Kususia kwake kulifanya Tuzo hiyo akabidhiwe Frederic Kanoute wa Mali.
Drogba alisusia kwa sababu sherehe hizo zilikuwa zinafanyika siku mbili tu kabla Nchi yake Ivory Coast ikutane na Guinea kwenye Robo Fainali ya Kombe la Afrika wakati huo fainali hizo za Kombe la Afrika zilikuwa zinachezwa Misri.
Badala yake alimtuma mkewe kumuwakilisha.
Licha ya kususa, alidai vilevile hataki kuhusishwa tena na Tuzo hiyo.
Vilevile, Drogba ameibua upya tena uhasama baada ya kuandika kwenye kitabu cha maisha yake kilichotolewa majuzi kwamba ingekuwa bora angempiga ngumi Beki wa Manchester United Nemanja Vidic kwenye Fainali ya UEFA CHAMPIONS LEAGUE wakati Chelsea waliposhindwa na Manchester United na kuukosa Ubingwa wa Klabu za Ulaya.
Drogba alilambwa kadi nyekundu kwenye mechi hiyo baada ya kuinua mkono na kumpiga kibao Vidic na hivyo kukosa kupiga penalti ambazo ziliizamisha timu yake Chelsea.
Didier Drogba pamoja na mwenzake wa Chelsea Michael Essien wa Ghana, Emmanuel Adebayor wa Togo na Arsenal, Wamisri Amr Zaki kutoka Klabu ya Zamalek ya Misri [kwa sasa yuko kwa mkopo Wigan] na Mohamed Aboutrika wa El Ahly ya Misri ndio watakaogombea TUZO YA MCHEZAJI BORA AFRIKA 2008.
STOKE CITY 2 TOTTENHAM 1

Bila shaka Meneja wa Tottenham Juande Ramos kijasho chembamba kinamtoka baada ya kupata kipigo kingine kwenye LIGI KUU na hivyo kuzidi kuipigilia misumari timu yake inayoshikilia mkia kwenye ligi baada ya kufungwa mabao 2-1 na Stoke City timu iliyopanda daraja msimu huu.
Mbali ya kipigo kwa Juande Ramos, vilevile Wachezaji wake wawili Gareth Bale na Michael Dawson, walibandikwa kadi nyekundu na mwingine Vedran Corluka ilibidi akimbizwe hospitali kwa ambyulensi baada ya kuumizwa kichwani tukio lililofanya mechi isimame kwa dakika 11.
Katika historia ya Tottenham, huo ndio mwanzo mbaya kabisa wa msimu kwani baada ya mechi 8 wameambulia pointi 2 tu na wako wa mwisho kabisa.
TUZO YA MCHEZAJI BORA ULAYA 2008 IITWAYO 'Ballon d'Or': LIGI KUU UINGEREZA ina Wachezaji 11 kati ya 30 wanaogombea!!!!!

Waendeshaji wa Tuzo ya 'Ballon d'OR', gazeti maarufu la soka liitwalo France Football Magazine, ambayo huzawadiwa kwa MCHEZAJI BORA WA ULAYA kila mwaka, wametangaza majina ya Wachezaji 30 wanaochezea Klabu mbalimbali Ulaya ambao watagombea zawadi hiyo.
Ballon d'Or maana yake ni MPIRA WA DHAHABU na ilianza kwa kutunukiwa kwa Wachezaji Bora Ulaya tangu mwaka 1956 na mwaka huo wa uzinduzi mshindi alikuwa Mchezaji mahiri sana wa Uingereza aliechezea Klabu ya Blackpool, Stanley Mathews.
Alieshinda tuzo hiyo mwaka 2007 ni Mchezaji wa AC Milan na Brazil, Kaka.
Kabla ya mwaka 2007, Mchezaji anaeweza kushinda tuzo hii ilikuwa ni lazima achezee Klabu iliyo Ulaya ambayo iko chini ya himaya ya UEFA na kabla ya 1995 ilikuwa ni lazima Mshindi awe ni Raia wa Nchi ya Ulaya.
Kati ya Wachezaji 30 watakaopigiwa kura na Waandishi wa Habari, Wachezaji 11 wanachezea LIGI KUU UINGEREZA na kati ya hao 11 watatu tu ndio Waingereza halisi kwa Uraia na ambao ni Wayne Rooney, Steven Gerrard na Frank Lampard.
SERIE A ya Italia ina Wachezaji watatu na LA LIGA ya Spain ina Washindani 11.
Mchezaji anaetegemewa sana kushinda Tuzo hii ya Ballon d'Or 2008 ni Cristiano Ronaldo wa Manchester United ambae pia ameshashinda Tuzo za Mchezaji Bora wa UEFA 2008 na LIGI KUU UINGEREZA.
Inategemewa Ronaldo atapata upinzani mkali kutoka kwa Mshindi wa tuzo hiyo 2007 Kaka wa AC Milan na Lionel Messi wa Barcelona.
Majina maarufu ambayo yamekuwa kama mtindo kila mwaka lazima yawepo kwenye listi hii, ambayo ni yale ya Thierry Henry na Ronaldinho, safari hii hayamo kabisa.

LISTI KAMILI [Klabu na Nchi wanazotoka]:

Emmanuel Adebayor (Arsenal), Togo; Sergio Aguero (Atletico Madrid), Argentina; Andrei Arshavin (Zenit St Petersburg), Russia ; Michael Ballack (Chelsea), Germany; Karim Benzema (Lyon), France; Gianluigi Buffon (Juventus), Italy; Iker Casillas (Real Madrid), Spain; Cristiano Ronaldo (Manchester United), Portugal; Didier Drogba (Chelsea), Ivory Coast; Samuel Eto'o (Barcelona), Cameroon; Cesc Fabregas (Arsenal), Spain; Fernando Torres (Liverpool), Spain; Steven Gerrard (Liverpool), England; Zlatan Ibrahimovic (Inter Milan), Sweden; Kaka (Milan AC), Brazil; Frank Lampard (Chelsea), England; Lionel Messi (Barcelona), Argentina; Pepe (Real Madrid), Portugal; Franck Ribery (Bayern Munich), France; Wayne Rooney (Manchester United), England; Marcos Senna (Villarreal), Spain; Sergio Ramos (Real Madrid), Spain; Luca Toni (Bayern Munich), Italy; Edwin van der Sar (Manchester United), Netherlands; Rafael van der Vaart (Real Madrid), Netherland; Ruud van Nistelrooy (Real Madrid), Netherlands; Nemanja Vidic (Manchester United), Serbia; David Villa (Valence CF), Spain; Xavi (FC Barcelone), Spain; Youri Zhirkov (CSKA Moscow), Russia.
Hull City waifunga West Ham na kuchupa hadi nafasi ya 3

Leo, timu iliyopanda daraja msimu huu Hull City mbele ya mashabiki wake kwenye Uwanja wa nyumbani wa KC, imezidi kuchanja mbuga baada ya kuwafunga wazoefu wa LIGI KUU West Ham ambao sasa wako chini ya Meneja Gianfranco Zola bao 1-0 na hivyo kushika nafasi ya 3 katika msimamo wa LIGI KUU.
Mpaka sasa, Hull City wamecheza mechi 8 na wana pointi 17, Arsenal wako wa 4 wakiwa wamecheza mechi 8 na wana pointi 16 huku Mabingwa Man United wako wa 5 na wana pointi 14 kwa mechi 7 walizocheza.
Hii ni mechi ya tatu mfululizo kwa Hull City kushinda ingawa mbili za kabla walishinda ugenini baada ya kuzipiga Arsenal 2-1 na Tottenham 1-0.
Mpaka mapumziko mechi ilikuwa dro na West Ham ndio waliotawala na kukosa mabao mengi.
Dakika tano tu ya kipindi cha pili, kona iliyopigwa na Andy Dawson ilitua kichwani kwa Michael Turner aliefunga bao la ushindi.
LIGI KUU: VIGOGO WAANZA KUJIKITA JUU!!!

Wanaongoza Chelsea wakifuatiwa na Liverpool, Arsenal na Man U!

Baada ya Chelsea, Liverpool na Arsenal kucheza mechi 8 kila mmoja huku Mabingwa Man U wakiwa wamecheza mechi moja pungufu, Chelsea ndie aliejikita katika uongozi wa LIGI KUU akiwa na pointi 20 sawa na Liverpool lakini Chelsea anaongoza kwa idadi kubwa ya magoli.
Wote, Chelsea na Liverpool, hawajapoteza hata mechi moja ingawa wote wametoka suluhu mechi mbili.
Timu hizi zitakutana uso kwa uso wiki ijayo wakati zitakapopambana Jumapili tarehe 26 Oktoba 2008, Stamford Bridge ambayo ni ngome ya Chelsea.
Anaefuata katika msimamo wa ligi ni Arsenal mwenye pointi 16 na tayari ameshafungwa mechi 2 na kutoka suluhu moja.
Mabingwa wa LIGI KUU, Manchester United, wako nafasi ya nne na wamecheza mechi moja pungufu na wana pointi 14.
Mechi ambayo bado wanayo mkononi na ambayo hawajaicheza ni ile dhidi ya Fulham iliyotakiwa ichezwe nyumbani kwa Man U, Old Trafford, lakini iliahirishwa kwa sababu Man U alikuwa kwenye mechi ya UEFA SUPER CUP waliyocheza na Zenit St Petersburg.
Mechi hii kiporo bado haijapangwa tarehe.
Endapo Man U watacheza hiki kiporo na kushinda basi watashika nafasi ya 3 na kuwa nyuma ya Chelsea na Liverpool kwa pointi 3 tu.
Leo, Timu mpya msimu huu iliyopanda daraja na inayostaajabisha wengi, Hull City, hasa baada ya kuzipiga Arsenal na Tottenham zote zikiwa nyumbani kwao, inashuka dimbani kupambana na West Ham inayosuasua.
Hull City wakishinda mechi ya leo dhidi ya West Ham, mechi inayochezwa kwake Uwanja wa KC, basi atakuwa na pointi 17 na atachupa hadi nafasi ya 3 na kuzipiku Arsenal na Man U ingawa kwa Man U atakuwa amemzidi mchezo mmoja.
Mechi nyingine inayochezwa leo ni ile ya Timu zinazoshika mkia, Stoke City iliyo nafasi ya 19 wakiwa na pointi 4 na Tottenham walio nafasi ya 20 na ya mwisho wakiwa na pointi 2 tu.
Mechi hii inachezewa Uwanja wa Britannia nyumbani kwa Stoke City.
MECHI ZA LEO: JUMAPILI, 19 Oktoba 2008

Hull City v West Ham [saa 11 jioni]

Stoke City v Tottenham [saa 12 jioni]

JUMATATU, 20 Oktoba 2008

Newcastle v Man City [saa 4 usiku]

REFA MSAIDIZI MECHI YA ASTON VILLA V PORTSMOUTH APASULIWA KICHWANI!!!

Katika mechi ya jana kati ya Aston Vill na Portsmouth iliyochezwa Villa Park nyumbani kwa Aston Villa na kuisha kwa sare ya 0-0 Refa Msaidizi, yaani mshika kibendera, aitwaye Phil Sharp, alirushiwa sarafu iliyompasua kichwani juu ya jicho la kulia na kumfanya aanguke chini kwa mstuko.
Pichani Refa mkuu kwenye mechi hiyo Mike Riley anaonekana akimpangusa jeraha msaidizi wake Phil Sharp.
Tukio hilo lilitokea dakika za mwisho mwisho za mchezo na ikabidi mechi isimame ili Refa huyo atibiwe na baada ya kubandikwa plasta Phil Sharp aliendelea kuchezesha.
Mtuhumiwa wa kosa hilo hakujulikana na Polisi wakishirikiana na Wana Usalama wa Uwanja wanachunguza kamera zinazochukua picha hapo uwanjani ili kumbaini mhalifu.
Klabu ya Aston Villa imetangaza wakimgundua huyo mtu basi hataruhusiwa tena kuingia Villa Park maishani mwake.
Powered By Blogger